Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 2 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 18 2021-09-01

Name

Janejelly Ntate James

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JANEJELLY J. NTANTE Aliuliza:-

Serikali inawahimiza watumishi kujiendeleza kielimu, lakini baada ya kuhitimu wanapoomba kubadilisha kada huteremshwa vyeo na mishahara:-

Je, Serikali haioni ipo haja ya kuwaacha na mishahara yao ili kujiendeleza isiwe adhabu?

Name

Deogratius John Ndejembi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chamwino

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Janejelly James Ntante, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, imeendelea kutoa Miongozo mbalimbali kuhusu namna ya kuwabadilisha kada/kazi watumishi waliojiendeleza kitaaluma. Aidha, Serikali inatambua umuhimu wa watumishi kubadilishwa na kupangiwa kazi kulingana na taaluma zao. Hivyo, kupitia Waraka wa Barua Kumb. Na. C/AC.44/45/01/ A/83 ya tarehe 01 Desemba, 2009, Serikali iliweka utaratibu wa kufuata wakati wa kuwabadilisha kada watumishi waliojiendeleza kitaaluma ambapo kuna aina mbili za kubadilishwa kada bila kuathiri watumishi waliomo katika kada hizo.

(i) Kumbadilisha kazi mtumishi aliyejiendeleza na kupata sifa zinazompandisha hadhi kitaaluma, mfano Afisa Kilimo Msaidizi kuwa Afisa Kilimo. Watumishi wa aina hii hubadilishwa hadhi na kuingizwa katika kada mpya kwa kuzingatia cheo cha kuanzia cha kada mpya. Iwapo vyeo walivyokuwa navyo vilikuwa na mishahara mikubwa kuliko mishahara ya cheo walichopewa baada ya kubadilishwa, huombewa kibali cha kuendelea kulipwa mishahara waliyokuwa wakilipwa kama mishahara binafsi hadi watakapopandishwa vyeo vyenye mshahara mkubwa kuliko mishahara binafsi. Utaratibu huu pia unawahusu watumishi wa kada saidizi ambao taaluma walizo nazo hazina vyuo vinavyotoa Astashahada/Stashahada au Shahada katika fani wanazofanyia kazi mfano Walinzi na Wasaidizi wa Ofisi.

(ii) Aina ya pili ni kuwabadilisha kazi watumishi waliojiendeleza katika fani nyingine tofauti na zile walizoajiriwa nazo kwa lengo la kukidhi matilaba ya kazi (job satisfaction) bila kuzingatia mahitaji ya mwajiri. Hawa hulazimika kubadilishwa kazi na kuingizwa katika cheo na ngazi ya mshahara wa cheo kipya na hawastahili mishahara binafsi kutokana na kulinda ukuu kazini na kuwajengea uzoefu wa kazi mpya ambazo wamezichagua wenyewe.

Mheshimiwa Spika, kwa msingi huu, Serikali inasititiza watumishi wa umma kujiendeleza katika kada walizoajiriwa nazo ili kuimarisha ufanisi wa utendaji kazi na kuwa wabobezi katika fani zao. Aidha, watumishi wa umma wanaaswa kupata ushauri kwa waajiri wao wanapotaka kujiendeleza kwenye fani tofauti na wanazofanyia kazi. Waajiri wanao wajibu wa kutenga nafasi za kuwabadilisha kada wale waliojiendeleza katika fani zao ili kuhakikisha kuwa rasilimali hiyo muhimu inatumika ipasavyo. Aidha, waajiri wahakikishe kuwa wanawashauri vizuri watumishi wao kabla ya kubadilishiwa kada/kazi watumishi waliojiendeleza kwenye fani tofauti. Endapo kwa namna yoyote kuna suala ambalo lina mazingira tofauti na haya, mwajiri au mtumishi mwenyewe anaweza kuomba ufafanuzi kutoka katika Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora wakati wowote.

Mheshimiwa Spika, naomba kuwasilisha.