Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 2 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 16 2021-09-01

Name

Anton Albert Mwantona

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rungwe

Primary Question

MHE. ANTON A. MWANTONA Aliuliza: -

Je, ni lini Serikali itapima maeneo yote ya umma ikiwemo Shule, Vituo vya Afya na Zahanati kwa kutumia Sheria Na. 4 na Na. 5 ili kuondokana na matatizo ya migogoro ya mipaka kwa Wananchi, lakini pia kuondokana na hoja za ukaguzi ambazo zaidi ya asilimia 90 ya Halmashauri wanazipata?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, ninaomba kujibu Swali la Mheshimiwa Anton Albert Mwantona, Mbunge wa Jimbo la Rungwe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kuwa baadhi ya maeneo ya umma yaliyoainishwa na kutengwa kwa ajili ya utoaji wa huduma mbalimbali za umma zinazotolewa na Serikali Kuu na Mamlaka za Serikali za Mitaa hayajapimwa na kuwekewa alama zinazoonekana kwa urahisi. Hali hii husababisha migogoro ya mara kwa mara ya ardhi na uvamizi wa maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na changamoto hizo Serikali imezielekeza halmashauri zote nchini kutenga fedha kila mwaka katika bajeti zao kwa ajili ya kupima maeneo yote ya taasisi za umma zilizo chini ya mamlaka hizo; ikiwa ni pamoja na kuweka alama zinazoonekana kwa urahisi ili kuepusha migogoro ya ardhi na kuzuia uvamizi unaofanywa na baadhi ya wananchi. Serikali ilishatoa maelekezo haya kwa Tawala za Mikoa na Mamlaka za Serikali za Mitaa; hivyo nitumie fursa hii kuzisisitiza Mamlaka za Serikali za Mitaa kuhakikisha zinatenga fedha na kutekeleza maelekezo hayo. Ahsante sana.