Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 1 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 12 2021-08-31

Name

Tumaini Bryceson Magessa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busanda

Primary Question

MHE. TUMAINI B. MAGESSA Aliuliza:-

Je, Serikali imejipangaje katika kupanga matumizi bora ya ardhi kwa Vijiji vyote nchi nzima ili kuondokana na migogoro ya matumizi ya ardhi?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Bryceson Magessa Tumaini, Mbunge wa Busanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Upangaji wa Matumizi ya Ardhi Na. 6 ya Mwaka, 2007 Sura ya 116 Kifungu cha18, kimebainisha Mamlaka za Upangaji kuwa ni Halmashauri za Vijiji, Wilaya na Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi ya Ardhi, ngazi ya Taifa na Mkoa. Jukumu la uandaaji wa Mipango ya Matumizi ya Ardhi ya Vijiji ni la Halmashauri za Vijiji na Wilaya. Wizara ya Ardhi kupitia Tume ya Mipango ina jukumu la kuwajengea uwezo, kusimamia na kuratibu Mamlaka za Upangaji na sekta mbalimbali katika utekelezaji wa mipango hiyo.

Mheshimiwa Spika, ili kuondokana na migogoro ya matumizi ya ardhi, jitihada mbalimbali zimeendelea kuchukuliwa na Serikali ili kuhakikisha vijiji vyote nchini vinaandaliwa mipango ya matumizi ya ardhi. Jitihada hizo ni pamoja na zifuatazo: -

Kwanza, ni kutenga bajeti kuwezesha uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi nchini, kupitia Mamlaka za Upangaji na hivyo kuondokana na migogoro ya matumizi ya ardhi.

Pili, kushirikisha wadau mbalimbali wa kimkakati wa matumizi ya ardhi, kuwezesha uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi katika vijiji mbalimbali nchini.

Tatu, kuendelea kuhamasisha Halmashauri za Wilaya na Mikoa kutenga bajeti ya uandaaji wa mipango wa matumizi ya ardhi katika vijiji kwenye maeneo yao.

Nne, kushirikiana na vyuo vinavyofundisha masuala ya ardhi ikiwemo Chuo cha Ardhi, katika uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi katika Halmashauri mbalimbali nchini.

Tano, kubuni miradi ya kimkakati itakayowezesha uandaaji, utekelezaji na usimamizi wa mipango ya matumizi nchini.