Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 1 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 14 2021-08-31

Name

Daniel Awack Tlemai

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Karatu

Primary Question

MHE. DANIEL A. TLEMAI Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua mgogoro wa mpaka kati ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro na Kata ya Mbulumbulu katika Kijiji cha Lositete?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Daniel Awack Tlemai, Mbunge wa Karatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mgogoro wa mpaka kati ya Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro na Kata ya Mbulumbulu katika Kijiji cha Lositete ulidumu kwa muda mrefu. Mgogoro huu ulitatuliwa kwa kushirikiana na mamlaka mbalimbali za Serikali zikiwemo:-

(i) Kamati za Ulinzi na Usalama za Wilaya ya Karatu, Monduli na Ngorongoro;

(ii) Wataalam kutoka Ofisi ya Katibu Tawala Mkoa wa Arusha; na

(iii) Wataalam kutoka Ofisi ya Katibu Tawala ya Wilaya za Karatu, Monduli na Ngorongoro; na Wahifadhi kutoka Mamlaka ya Hifadhi Ngorongoro.

Mheshimiwa Spika, Mamlaka hizi zote zilishiriki kutafsiri GN iliyoanzisha mipaka ya maeneo hayo kisheria.

Mheshimiwa Spika, Kijiji cha Lositete kiko katika Wilaya ya Karatu na sio Wilaya ya Ngorongoro ambapo wananchi wa kutoka kijiji hicho walivamia eneo la Hifadhi ya Ngorongoro na taratibu za kuwaondoa zilifanyika na kuwarudisha katika maeneo yao. Pamoja na kuwa Sheria ya Hifadhi ya Ngorongoro inaruhusu matumizi mseto, sheria hii iliwekwa kwa ajili ya wenyeji waliomo ndani ya hifadhi. Aidha, ndani ya hifadhi pia kuna maeneo ambayo yanasimamiwa Serikali ili kulinda uoto wa asili likiwemo eneo hili.

Mheshimiwa Spika, niendelee kutoa msisitizo kwa jamii zote zinazozunguka mipaka ya hifadhi kuheshimu maeneo yote yaliyohifadhiwa kwa faida ya jamii na maslahi ya Taifa kwa ujumla. Ahsante.