Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 4 Education, Science,Technology and Vocational Training, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia 30 2021-04-06

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO K.n.y. MHE. RASHID A. SHANGAZI Aliuliza:-

Je, ni vigezo gani hutumika kushindanisha ufaulu kwa shule za msingi na sekondari kwa Halmashauri na Mikoa hapa nchini?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Spika, kwa vile na mimi ni mara yangu kwanza kusimama mbele ya Bunge lako tukufu toka uteuzi ulipofanyika, basi nichukue fursa hii adhimu na adimu kwanza kabisa kumshukuru sana Mwenyezi Mungu, Mungu ambaye ametuumba na akatujalia uhai, lakini shukrani ya pili kwa Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kutuamini katika Wizara hii kuendelea kuhudumu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huo sasa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Rashid Abdallah Shangazi, Mbunge wa Mlalo kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kigezo kinachotumika katika kuzipanga shule kwa ubora wa ufaulu katika Halmashauri na Mikoa kwenye mitihani ya kitaifa ni wastani wa alama kwa shule za msingi na ufaulu wa watahiniwa kimadaraja na kimasomo kwa shule za sekondari.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, mpangilio wa ubora wa ufaulu kwa Halmashauri na Mikoa hutegemea wastani wa ufaulu wa shule zilizopo katika Halmashauri au Mkoa husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, shule za msingi hupangwa katika mpangilio wa ubora wa ufaulu kwa kuzingatia kigezo cha wastani wa alama walizozipata watahiniwa wote wa shule husika katika masomo yote waliyoyafanya. Wastani huo hupatikana kwa kufuata hatua zifuatazo; kukokotoa jumla ya alama walizopata watahiniwa wote wa shule husika kwenye masomo yote waliyoyafanywa; na kukokotoa wastani wa alama wa shule kwa kugawanya jumla ya alama walizopata watahiniwa wote wa shule kwa idadi ya watahiniwa wa shule husika.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa upande wa shule za sekondari mpangilio wa ubora wa ufaulu huzingatia kigezo cha wastani wa ufaulu (Grade Point Average-GPA) wa watahiniwa kimadaraja na kimasomo. Wastani huo hupatikana kwa kukokotoa wastani wa ufaulu wa watahiniwa wa shule husika kimadaraja na kimasomo. Jumla ya wastani huo wa ufaulu wa shule wa kimasomo na kimadaraja hukokotolewa tena ili kupata ubora wa ufaulu kwa kila shule. Ahsante!