Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 4 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 22 2021-04-06

Name

Neema Gerald Mwandabila

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NEEMA G. MWANDABILA Aliuliza: -

(a) Je, ni lini Serikali itapeleka watumishi na vifaa muhimu kwenye hospitali inayojengwa katika Mji wa Tunduma ili ianze kufanya kazi mapema?

(b) Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza madaktari na wakunga pamoja na kuongeza bajeti katika Kituo cha Afya cha Tunduma ili kukidhi mahitaji ya kituo?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza kusimama hapa tangu Mheshimiwa Rais aliponipa dhamana ya kumsaidia kama Naibu Waziri, Ofisi ya Rais - TAMISEMI, naomba nitumie nafasi hii kumshukuru sana Mheshimiwa Rais, lakini nimuahidi kwamba nitafanya kazi kwa nguvu zangu zote. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema Gerald Mwandabila, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo: -

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inaendelea na ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Mji Tunduma ambayo ilianza kujengwa katika mwaka wa fedha 2016/2017. Ujenzi wa awamu ya kwanza unahusisha jengo la ghorofa moja lenye sehemu tisa za huduma mbalimbali za OPD ambalo limetumia shilingi bilioni nne ambalo hadi Machi, 2021 ujenzi wake umefikia asilimia 82.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022, Serikali itaomba kuidhinishiwa shilingi bilioni moja kwa ajili ya kukamilisha ujenzi na shilingi milioni 500 kwa ajili ya ununuzi wa vifaa tiba. Baada ya kukamilisha ujenzi huo Serikali itapeleka watumishi na huduma za OPD zitaanza kutolewa. Serikali imeshawapanga madaktari wawili katika hospitali hii ambao kwa sasa wanaendelea kutoa huduma kwenye Kituo cha Afya Tunduma wakisubiri kukamilika kwa Hospitali ya Halmashauri ya Mji wa Tunduma.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Afya Tunduma kina jumla ya watumishi 74 kati ya watumishi 52 wanaohitajika katika ngazi ya kituo cha afya na hivyo kuwa na ziada ya watumishi 22. Idadi ya watumishi waliozidi inatokana na kituo hiki kutumika kama Hospitali ya Mji wa Tunduma. Hivyo, watumishi hawa watahamishiwa katika hospitali mpya ya mji mara itakapokamilika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika mwaka wa fedha 2021/2022 Serikali itaomba kuindhinishiwa shilingi milioni 409 kwa ajili ya dawa na vifaa tiba katika Kituo cha Afya cha Tunduma ambalo ni ongezeko la shilingi milioni 84 ikilinganishwa na bajeti ya shilingi milioni 325 iliyoidhinishwa katika bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021.