Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 2 Education, Science,Technology and Vocational Training, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia 17 2021-03-31

Name

Husna Juma Sekiboko

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HUSNA J. SEKIBOKO Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani kwa vijana wanaoshindwa mitihani kwenye ngazi mbalimbali za elimu nchini?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA Alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Husna Juma Sekiboko, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inatambua umuhimu wa kuwaendeleza vijana wakiwemo wale ambao hawakubahatika kuendelea na ngazi ya elimu inayofuata ya masomo baada ya kuhitimu. Hii ni kwa sababu vijana hawa ndiyo rasilimaliwatu ya Taifa inayotegemewa katika maendeleo ya viwanda na uchumi wa kati.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ina mipango mbalimbali ya kuwaendeleza vijana hao. Mipango hiyo ni pamoja na ujenzi wa Vyuo vya VETA katika ngazi za Mikoa na Wilaya pamoja na ukarabati wa Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi. Kwa mfano, katika kipindi cha mwaka 2020/ 2021, Serikali imeendelea na ujenzi wa vyuo vipya vya VETA 29 katika ngazi ya Wilaya ambavyo vinatarajiwa kukamilika mwezi Juni 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile, Serikali imeendelea na ukarabati na ujenzi wa miundombinu katika Vyuo vya Maendeleo ya Wananchi 54 kwa lengo la kuwezesha wananchi na vijana kupata ujuzi mbalimbali. Aidha, vipo vyuo 34 vya Wilaya na 22 vya Mikoa ambavyo vinadahili wanafunzi katika fani mbalimbali na hivyo kutoa fursa kwa vijana hao kujiendeleza na kupata ujuzi mbalimbali.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kutumia fursa hii kuwaomba wazazi na Watanzania kwa ujumla kutumia vyuo hivyo ili kuwawezesha vijana na wananchi wengine kujiendeleza na kupata ujuzi katika fani mbalimbali. Ahsante.