Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 9 Water and Irrigation Wizara ya Maji 124 2021-02-12

Name

George Natany Malima

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Primary Question

MHE. GEORGE N. MALIMA Aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kutatua tatizo la muda mrefu la uhaba wa maji kwa wananchi wa Mji wa Mpwapwa?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa George Natany Malima, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua tatizo la muda mrefu la uhaba wa maji katika mji wa Mpwapwa. Katika kutatua tatizo hilo, mikakati ya muda mfupi na muda mrefu imekuwa ikitekelezwa. Kwa upande wa mikakati ya muda mfupi, mwaka 2020/2021 Serikali imetenga fedha kiasi cha shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuchimba visima virefu viwili katika eneo la Kikombo. Ujenzi wa bomba kuu kutoka katika visima hivyo viwili mpaka katika tanki la Vingh’awe, kuongeza mtandao wa maji katika maeneo ya pembezoni ambayo ni Vijiji vya Vingh’awe na Behero. Aidha, kazi nyingine itakayofanyika ni kufunga pampu mpya kwenye kisima cha Kikombo ambacho kitaongeza uzalishaji wa maji katika kisima hicho kutoka lita 40,000 kwa saa hadi lita 65,000 kwa saa. Kukamilika kwa kazi hizi kutaboresha upatikanaji wa huduma ya maji katika mji wa Mpwapwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa mpango wa muda mrefu, Serikali kupitia Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira ya Mpwapwa kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maji ya Dodoma (DUWASA) inaendelea kufanya usanifu unaotarajiwa kukamilika mwezi Mei, 2021 na kubainisha maeneo ambayo yana upungufu mkubwa wa maji katika Mji wa Mpwapwa ambapo vitachimbwa visima virefu vinne na kuongeza mtandao wa mabomba katika Mji wa Mpwapwa na viunga vyake. Aidha, katika mwaka 2021/2022, Serikali itakarabati mradi wa maji wa mtiririko wa Mayawile na Kwamdyanga.