Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 8 Education, Science,Technology and Vocational Training, Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia 108 2021-02-11

Name

Mwanaisha Ng'anzi Ulenge

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ENG. MWANAISHA N. ULENGE Aliuliza:-

Miradi mikubwa ya ujenzi nchini inafanywa na kampuni kutoka Bara la Asia wakati wahandisi nchini wanasoma uhandisi kwa mitaala ya Uingereza na Marekani.

(a) Je, Serikali haioni haja ya kuongeza mitaala ya Asia katika mitaala ya Vyuo vya Uhandisi ili Wahandisi wetu wapate utaalam katika miradi ya ujenzi?

(b) Je, suala la kubadilishana weledi limepewa kipaumbele gani katika miradi inayoendelea kujengwa hapa nchini?

Name

Omary Juma Kipanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mafia

Answer

NAIBU WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Engineer Mwanaisha Ng’anzi Ulenge, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Uhandisi ni fani ya Kimataifa ambayo mitaala yake haitofautiani kijiografia. Kwa muktadha huo mitaala ya shahada za uhandisi katika vyuo vyetu nchini nayo ni ya viwango vya kimataifa. Hata hivyo, ni kawaida kuhuisha mitaala mara kwa mara ili kuingiza utaalam mpya kwenye fani. Hivyo basi ni nia ya Serikali yetu kuhuisha (review and update) ya mitaala ya kihandisi na fani nyingine za kipaumbele kwenye Tanzania ya viwanda kama tunavyoongozwa na Ilani ya Chama cha Mapinduzi 2020 – 2025, Ibara ya 80 Ukurasa 130 Kipengele (c) ambayo inaagiza “kuhuisha Mitaala (curriculum review) na kuanzisha programu kulingana na mahitaji ya Kitaifa, Kikanda na Kimataifa ili wahitimu wawe na stadi stahiki za kumudu kufanya kazi mbalimbali za kuajiriwa na kujiajiri na hasa kwa kuzingatia Mapinduzi ya Nne ya Viwanda”.

(b) Mheshimiwa Spika, suala la kubadilishana uweledi wa kihandisi kati ya miradi mikubwa inayoendelea tayari linatekelezwa ambapo wahitimu wetu wa uhandisi hupata nafasi za utarajali katika miradi yetu mikubwa ya Kitaifa ili kupata weledi. Kwa mfano, kupitia Bodi ya Usajili wa Wahandisi (Engineers Registration Board) wapo wahandisi wahitimu 197 ambao wanashiriki kwa sasa katika miradi mikubwa mbalimbali mfano Mradi Umeme wa Mwalimu Nyerere na Mradi wa Reli ya Mwendo Kasi. Hivyo, Serikali itaendelea kuweka mfumo wa kuhakikisha kuwa katika miradi mikubwa inayotekelezwa nchini suala la kubadilishana uweledi linaendelea kupewa kipaumbele. Ahsante.