Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 8 Energy and Minerals Wizara ya Madini 106 2021-02-11

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA Aliuliza:-

Je, ni lini uzalishaji wa madini ya niobium utaanza katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya?

Name

Prof. Shukrani Elisha Manya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Jimbo la Mbeya Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, mradi wa uchimbaji wa madini ya niobium katika Wilaya ya Mbeya unahusisha leseni tatu za uchimbaji wa kati na eneo hili lina jumla ya kilometa za mraba 22.1. Mradi huu unatarajiwa kuwa na uhai wa miaka 30 na unamilikiwa na Kampuni ya Panda Hill Tanzania, ambayo ni kwa ubia wa 50:50 na kampuni za Cradle Resources Limited na Tremont Investments. Mradi huu utahusisha uchimbaji wa madini ya niobium ambayo yataongezwa thamani nchini kwa kuchanganywa na madini ya chuma ili kuwa na mchanganyiko wa madini ya FerroNiobium, zao hili ndilo lenye soko katika nchi za Ulaya, Asia na Amerika ya Kaskazini.

Mheshimiwa Spika, Mwekezaji aliwasilisha Wizarani maombi ya misamaha ya kodi katika uwekezaji wake. Mwekezaji alielekezwa na Wizara kufuata matakwa ya Sheria ya Madini ambayo ndiyo inayotumiwa na wawekezaji wengine wote katika Sekta ya Madini.

Mheshimiwa Spika, nitoe rai kwa mwekezaji kukamilisha taratibu za kumwezesha kuanza utekelezaji wa mradi ikiwepo pia kupata ridhaa ya maandishi kutoka kwa wamiliki wa maeneo katika leseni zake kama ilivyo Sheria ya Madini. Ahsante.