Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 7 Water and Irrigation Wizara ya Maji 101 2021-02-10

Name

Eng. Ezra John Chiwelesa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Primary Question

MHE. ENG. EZRA J. CHIWELESA Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa mradi wa kutoa maji toka Ziwa Victoria kuyapeleka Biharamulo kama Mheshimiwa Rais alivyoahidi hapo tarehe 16/09/2020 alipokuwa Biharamulo katika Kampeni za Uchaguzi Mkuu, 2020?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maji, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Eng. Ezra John Chiwelesa, Mbunge wa Biharamulo Magharibi, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto za upatikanaji huduma ya maji katika Wilaya ya Biharamulo. Hivyo, katika bajeti ya mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali inatekeleza mradi wa upanuzi wa mtandao wa maji wenye urefu wa km 10.9 katika maeneo ya Ng’ambo, Kalebezo, Nyakatuntu, Rubondo Chuoni na Rukaragata na kuchimba kisima katika eneo la Rukagarata. Thamani ya mradi huu ni shilingi milioni 178.9 na utekelezaji wa mradi umefikia asilimia 70.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na changamoto ya uhaba wa maji katika Mji wa Biharamulo, Serikali iliamua chanzo cha uhakika cha maji kiwe Ziwa Victoria badala ya bwawa na chemichemi vinavyotumika kwa sasa. Hivyo mradi wa usambazaji maji katika Mji wa Biharamulo ambao utatoa maji katika Ziwa Victoria umefikia katika hatua ya kuandaa makabrasha ya zabuni (tender documents). Utekelezaji utaanza katika mwaka wa fedha 2021/2022.

Aidha, kupitia Mradi wa Maziwa Makuu, Wilaya ya Biharamulo itanufaika kupitia chanzo cha Ziwa Victoria ambapo jumla ya vijiji 12 vya Rwekubo, Rusese, Kabindi, Runazi, Rukora, Kikomakoma, Kagoma, Songambele, Kasozibakaya, Nyamigogo, Chebitoke na Nyabusozi vitapata huduma ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali itaendelea kutekeleza miradi ya maji kulingana na upatikanaji wa fedha.