Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 7 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 90 2021-02-10

Name

Silvestry Fransis Koka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Mjini

Primary Question

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE (K.n.y. MHE. SILVESTRY F. KOKA) Aliuliza:-

Miundombinu ya maji katika Shirika la Elimu Kibaha ilijengwa miaka 50 iliyopita kwa kutumia mabomba ya Asbestos ambayo siyo rafiki kwa afya za binadamu, lakini pia ni chakavu sana:-

(a) Je, ni lini Serikali itatatua changamoto ya maji katika shirika hilo?

(b) Je, ni lini Serikali itakarabati majengo ya Chuo cha FDC katika Shirika hili?

Name

Dr. Festo John Dugange

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Wanging'ombe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DKT. FESTO J. DUGANGE) Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais,TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Silvestry Francis Koka, Mbunge wa Kibaha Mjini, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali inatambua changamoto ya maji katika Shirika la Elimu Kibaha inayotokana na miundombinu mibovu na ya muda mrefu ambayo ni kutokana na uwepo wa mabomba ya maji ya kipenyo cha milimita 200 yenye urefu wa kilomita nne na kipenyo cha milimita 150 yenye urefu wa kilomita mbili yaliyojengwa kwa asbestos tangu kuanzishwa kwa Shirika hili.

Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, Serikali ilikwishabadilisha bomba la asbestos lenye urefu wa kilomita 0.75 la kipenyo cha milimita 200 na bomba lenye urefu wa kilomita moja na kipenyo cha milimita 150 kuwa PVC. Serikali itaendelea kubadilisha mabomba hayo kulingana na upatikanaji wa fedha. Aidha, Shirika linaendelea kufanya matengenezo madogo madogo kwa kutumia mapato ya ndani pindi uharibifu unapotokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kwa kutambua umuhimu wa shirika hili, imekamilisha ukarabati wa Shule ya Sekondari Kibaha kwa gharama ya Shilingi bilioni 1.6. Vilevile katika mwaka wa fedha 2020/2021, Serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni 80 kwa ajili ya ujenzi wa bweni katika Shule ya Sekondari ya Wasichana Kibaha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imefanya tathmini ya ukarabati wa miundombinu ya majengo ya Chuo cha Maendeleo ya Wananchi cha Shirika la Elimu Kibaha ambapo kiasi cha shilingi bilioni 1.48 kinahitajika ili kufanya matengenezo. Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya kufanya ukarabati. Hata hivyo, Shirika la Elimu Kibaha lilifanya ukarabati mdogo wa madarasa na jengo la utawala kwa kutumia mapato ya ndani ambao uligharimu shilingi milioni 25.73.