Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 6 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 87 2021-02-09

Name

Felista Deogratius Njau

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FELISTA D. NJAU Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itatoa hati kwa Wananchi wa Meko na Basihaya baada ya maeneo hayo kupimwa?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Felista Deogratius Njau, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Meko liko katika Kata ya Kunduchi Manispaa ya Kinondoni awali eneo hilo lilitengwa kwaajili ya machimbo ya kokoto. Baada ya machimbo kufungwa Manispaa ilidhamiria kupima viwanja kwa ajili ya Kituo cha Biashara. Hata hivyo upimaji haukufanyika kutokana na eneo hilo kuwa limevamiwa na wananchi. Mwaka 2017 Manispaa ya Kinondoni ilimaliza mgogoro na wavamizi kwa kuruhusu wananchi wapimiwe viwanja katika eneo hilo kupitia mpango wa urasimishaji wa makazi.

Mheshimiwa Naibu Spika, aidha ilikubalika kuwa wananchi watapimiwa viwanja katika maeneo yale waliyoyaendeleza na maeneo yaliyo wazi yatapangwa na kupimwa viwanja vya matumizi ya umma. Kazi ya upimaji ilianza tarehe Mosi Januari, 2019 na kukamilika tarehe 20 Januari, 2021 na jumla ya viwanja 840 vimepimwa na hatua ya umilikishaji zinaendelea.

Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Basihaya lipo katika Kata ya Bunju, Mtaa wa Basihaya ambako kuna Vitongoji vya Chasimba, Chatembo, Chachui ambavyo kwa sehemu kubwa uendelezaji wake umefanywa ndani ya ardhi inayomilikiwa na Kiwanda cha Saruji cha Wazo. Wamiliki wa Kiwanda cha Wazo walipeleka malalamiko Mahakamani baada ya kuona eneo lao limevamiwa. Mahakama kupitia Shauri Na. 129 la mwaka 2008 kati ya Haruna Mpangao na wenzake 932 dhidi ya Tanzania Portland Cement ilitoa uamuzi kuwa wananchi waliovamia katika eneo hilo waondolewe.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara ya Ardhi ilichukua jitihada za kufanya majadiliano na mwekezaji ili kuangalia namna bora ya kutatua mgogoro huo ambapo iliamua wananchi walioendeleza katika maeneo hayo wasiondolewe bali walipe gharama ambazo atapewa mwekezaji ili akanunue eneo lingine kwa ajili ya kupata malighafi za kutengeneza saruji.

Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali imeshawapimia viwanja waendelezaji wote katika eneo hilo ambapo jumla ya viwanja 4,000 vimepatikana na kila mwendelezaji atatakiwa kulipia gharama zitakazotumika kumlipa mmiliki wa kiwanda. Wizara inaendelea kufanya majadiliano na mmiliki wa Kiwanda cha Saruji cha Wazo kuhusu gharama na fidia ya eneo lililoendelezwa na wananchi.