Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 6 Good Governance Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 76 2021-02-09

Name

Neema Kichiki Lugangira

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NEEMA K. LUGANGIRA Aliuliza:-

Kumekuwa na malalamiko kutoka kwa wananchi wa Manispaa ya Bukoba kuwa wanufaika wa TASAF ni wananchi wenye uwezo badala ya kaya maskini:-

Je, hayo ndiyo malengo ya kuanzishwa kwa TASAF?

Name

Deogratius John Ndejembi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chamwino

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA Alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa nami ndiyo mara yangu ya kwanza kusimama mbele ya Bunge lako hili Tukufu, napenda kuanza kwa kumshukuru Mungu kwa mema yote ambayo anaendelea kutujalia hadi kufika siku hii ya leo. Pili, napenda kutoa shukrani zangu za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais, Dkt. John Pombe Joseph Magufuli, kwa imani yake kwangu na kuniteua kuwa Naibu Waziri katika ofisi yake.

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Neema Kichiki Lugangira, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, malengo ya Mpango wa TASAF ni kuzinusuru kaya maskini katika Halmashauri zote za Tanzania Bara na Unguja na Pemba kwa upande wa Zanzibar.

Mheshimiwa Naibu Spika, awamu ya kwanza ya Mradi wa Kunusuru Kaya Maskini ulianza rasmi mwaka 2000 hadi 2005; awamu ya pili ilianza mwaka 2005 hadi 2012; na awamu ya tatu, kipindi cha kwanza ilianza kutekelezwa mwaka 2013 hadi Desemba, 2019; na kipindi cha pili cha awamu ya tatu kilianza Februari, 2020 hadi Septemba, 2023 ambapo jumla ya kaya maskini 1,100,000 zimeweza kuandikishwa na wanufaika kunyanyua hali yao ya kimaisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika Mkoa wa Kagera jumla ya kaya maskini 68,915 zimeandikishwa na kuingizwa kwenye Mpango huu wa TASAF. Katika utekelezaji wa kipindi cha kwanza walengwa wamepokea ruzuku kwa takribani miaka mitano. Hali hii imechangia walengwa hawa kuwa na miradi mikubwa ya uzalishaji mali kama mashamba, mifugo na shughuli za ujasiriamali ambazo zimewawezesha wao kuboresha maisha na kujiimarisha kiuchumi. Walengwa kama hao ndio wanalalamikiwa kuwa TASAF inasaidia watu wenye uwezo badala ya kaya maskini. Ukweli ni kwamba kaya hizo ziliingia kwenye mpango zikiwa na hali duni na ziliweza kujikwamua kiuchumi.