Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 5 Works, Transport and Communication Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi 72 2021-02-08

Name

George Natany Malima

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Primary Question

MHE. GEORGE N. MALIMA Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaanza ujenzi wa barabara ya kuanzia Njia Panda ya Kongwa hadi Mpwapwa Mjini yenye urefu wa takribani kilometa 30 ambayo ipo katika Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2020 – 2025?

Name

Eng. Godfrey Msongwe Kasekenya

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ileje

Answer

NAIBU WAZIRI WA UJENZI NA UCHUKUZI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa George Natany Malima, Mbunge wa Mpwapwa, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ujenzi wa barabara ya Njia Panda ya Kongwa hadi Mpwapwa ulianza kutekelezwa kwa kujengwa kwa kiwango cha lami kuanzia mwaka wa fedha 2013/2014. Ujenzi huu ulianza baada ya kukamilika kwa kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina mwaka 2013 uliohusisha barabara ya Mbande – Kongwa Junction. Kongwa Junction – Ugogoni kilometa 17.5, Kongwa Junction – Mpwapwa – Ving’awe kilometa 38.85 na Mpwapwa – Gulwe – Kibakwe kilometa 46.93.

Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilika kwa kazi ya upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, ujenzi kwa kiwango cha lami ulianza, ambapo hadi sasa ujenzi wa sehemu ya Barabara ya Mbande – Kongwa Junction kilometa 16.7 umekamilika. Serikali kwa sasa inaendelea na ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Njia Panda ya Kongwa hadi Mpwapwa. Katika mwaka wa fedha huu tunaondelea nao Serikali imetenga shilingi bilioni 4.95 kwa ajili ya kuendelea na ujenzi kwa kiwango cha lami katika mji wa Mpwapwa. Ujenzi kwa kiwango cha lami wa barabara ya Njiapanda ya Kongwa hadi Mpwapwa utaendelea kutekelezwa kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali imeendelea kutenga fedha za matengenezo mbalimbali ya barabara hizi ili ziendelee kupitika majira yote ya mwaka. Katika mwaka huu wa fedha 2020/2021 jumla ya shilingi bilioni 1.1 zimetengwa kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Pandambili – Saguta – Mpwapwa – Ng’ambi na shilingi milioni 751.596 kwa ajili ya matengenezo ya barabara ya Manchali – Ng’ambi – Kongwa Junction – Hogolo Junction ambapo barabara ya Njiapanda ya Kongwa hadi Mpwapwa imezingatiwa. Ahsante.