Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 5 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 62 2021-02-08

Name

Daniel Baran Sillo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Primary Question

MHE. SILLO D. BARAN Aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itamaliza migogoro ya mipaka kati ya Hifadhi ya Tarangire na Vijiji vya Gijedabung, Ayamango, Gedamar na Mwada katika Jimbo la Babati Vijijini?

Name

Mary Francis Masanja

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII Alijibu: -

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Sillo Daniel Baran, Mbunge wa Jimbo la Babati Vijijini, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ilihakiki mpaka wa Hifadhi ya Taifa Tarangire mwaka 2004 kwa kutumia Tangazo la Serikali Na. 160 la tarehe 19 Juni, 1970 ambapo alama za mipaka ziliwekwa ardhini. Kazi hiyo ilifanywa na wataalam kutoka Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi.

Mheshimiwa Spika, uhakiki huo ulibainisha kuwa: (i) hifadhi ilikuwa imechukua baadhi ya maeneo ya Vijiji vya Mwikantsi (Hekta 1,014) na Sangaiwe, Kata ya Mwada (Hekta 536), hivyo maeneo haya yalirejeshwa kwa wananchi. (ii) wananchi pia, walichukua maeneo ya hifadhi katika Vijiji vya Ayamango (Hekta 2,986.3), Gedamar ( Hekta 2,185.1), Gijedabung (Hekta 1,328.2), Quash (Hekta 1,587.9) na Orng’andida (Hekta 930.6) ambavyo vimerejeshwa.

Mheshimiwa Spika, katika Vijiji vya Quash na Orng’ndida maeneo yaliyoangukia ndani ya mpaka wa hifadhi hayakuwa na watu, hivyo ilikuwa rahisi kuyarejesha hifadhini. Upande wa maeneo ya Vijiji vya Ayamango, Gedamar na Gijedabung uthamini wa mali za wananchi ambao walikuwa ndani ya mpaka wa hifadhi ulifanyika. Jumla ya kiasi cha shilingi za Kitanzania 175,050,924 zililipwa kwa wananchi hao kama fidia ya mali, posho ya usumbufu, posho ya makazi na posho ya usafiri kwa wote waliotakiwa kuhama. Malipo hayo ya fidia yalifanyika kama ilivyokuwa imepangwa na wananchi waliondoka ndani ya hifadhi.