Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 2 Water and Irrigation Wizara ya Maji 24 2021-02-03

Name

Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA Aliuliza: -

Mji wa Mwanhuzi unakabiliwa na tatizo kubwa sana la maji safi na salama kutokana na chanzo chake cha maji cha bwawa la Mwanyahina kujaa tope: -

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuhakikisha wananchi wa Mji wa Mwanhuzi na vitongoji vyake wanapata maji safi na salama ya kutosha kwa mwaka mzima?

Name

Maryprisca Winfred Mahundi

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAJI alijibu: -

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Leah Jeremiah Komanya, Mbunge wa Jimbo la Meatu, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mji wa Mwanhuzi, Wilayani Meatu unategemea chanzo kimoja cha Maji ambacho ni Bwawa la Maji la Mwanyahina. Bwawa hilo lilijengwa mwaka 1999 lenye uwezo wa kuhifadhi maji mita za ujazo millioni 1.6. Bwawa hili kwa sasa limejaa tope jingi na kusababisha kupungua kina cha kuhifadhi maji kutoka kina cha mita 9 hadi mita 5 zinazohifadhi maji kwa matumizi ya wakazi wa Mji wa Mwanhuzi na vijiji jirani.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika kuboresha huduma ya maji katika mji wa Mwanhuzi na vitongoji vyake, Serikali imekamilisha utafiti, usanifu na kuanza kutekeleza ujenzi wa chanzo mbadala cha ukusanyaji na usafirishaji wa maji kutoka bonde la Mto Semu hadi kwenye matanki yanayotumika kusambaza maji katika Mji wa Mwanhuzi. Gharama za mradi huo shilingi milioni 742. Tayari Serikali imetuma kiasi cha shilingi milioni 276.6 kwa ajili ya kazi hizo za ujenzi wa mradi mbadala wa kutoa maji katika bonde la Mto Semu na kuyapeleka mjini Mwanhuzi. Mradi huu unatarajiwa kukamilika mwezi Julai, 2021.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa lengo la kutatua tatizo la muda mrefu katika mji wa Mwanhuzi na vitongoji vyake, Serikali ipo katika hatua za awali za kutekeleza mradi mkubwa wa kutoa maji kutoka Ziwa Victoria unaolenga kumaliza changamoto za huduma za maji katika mkoa wa Simiyu zikiwemo Wilaya za Busega, Bariadi, Maswa, Itilima na Meatu.