Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 1 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 1 2021-02-02

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. BONIFACE M. GETERE aliuliza:-

Je, Serikali inachukua hatua gani endelevu za kuondoa tatizo sugu la upungufu wa madawati kwenye baadhi ya shule za msingi na sekondari nchini?

Name

David Ernest Silinde

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduma

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE) alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kabla sijaanza kujibu swali namba moja la Mheshimiwa Mwita Getere, naomba kwa idhini yako nitoe shukrani kwanza kwa Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kushinda uchaguzi, lakini vilevile kuweza kuingia ndani ya Bunge. Pia kwa kipekee kabisa nimshukuru sana Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa imani kubwa ambayo amenionesha kwangu mpaka kuniteua kuwa Naibu Waziri katika Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambayo nahudumu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, vilevile naomba nikishukuru chama changu Chama Cha Mapinduzi kwa imani yake kubwa ambayo wameionesha kwangu kwa kunipa nafasi ya kugombea na mwisho wa siku kunisaidia kampeni na kushinda kwa kishindo. Nakishukuru sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa kipekee kabisa niishukuru familia yangu. Mama yangu mzazi kwa kuwa nami katika kipindi chote mpaka kufikia hatua hii ambayo leo nimefikia…

SPIKA: Sasa majibu!

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. DAVID E. SILINDE): Mheshimiwa Spika, sasa naomba nijibu swali la Mheshimiwa Mwita Getere, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI naomba kujibu swali la Mheshimiwa Boniface Mwita Getere, Mbunge wa Bunda kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, changamoto ya wanafunzi kukosa madawati katika shule za msingi na sekondari imetokana na mwitikio mkubwa wa wazazi kuandikisha wanafunzi shuleni baada ya Serikali kuanzisha mpango wa utoaji wa elimu bila malipo ambapo idadi ya wanafunzi wanaoandikishwa kwenye shule za msingi na sekondari umeongezeka maradufu.

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutoa fedha kwa ajili ya ununuzi wa madawati ambapo mpaka sasa mwaka 2015 kulikuwa na madawati 3,024,311 na mpaka sasa hivi kufikia mwezi Septemba 2020 Serikali imeongeza madawati kufikia madawati 8,095,207 ambapo kumekuwa na ongezeko la madawati 5,070,899.

Mheshimiwa Spika, katika kukabiliana na upungufu wa madawati, Serikali imeendelea kuchukua hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na kutenga fedha kwa ajili ya utengenezaji wa madawati kwenye miradi yote inayotengewa fedha za ukamilishaji wa vyumba vya madarasa kwa shule za msingi na sekondari na kuhamasisha wananchi na kuwashirikisha wadau na asasi mbalimbali katika utengenezaji wa madawati pamoja na kuendelea kutenga fedha ya matengenezo ya madawati kwenye Halmashauri kupitia mapato ya ndani. Nashukuru sana.