Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 19 Sitting 3 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 23 2020-04-02

Name

Aida Joseph Khenani

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENAN aliuliza:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kupeleka fedha kwenye kivutio cha maporomoko ya Kalambo?

Name

Dr. Hamisi Andrea Kigwangalla

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nzega Vijijini

Answer

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Joseph Khenan, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, maporomoko ya Mto Kalambo yapo katika Msitu wa Hifadhi ya Mazingira Asilia Kalambo yenye ukubwa wa hekta 41,958. Hifadhi hii ni muunganiko wa misitu miwili; Msitu wa Mto Kalambo na Msitu wa Hifadhi wa Maporomoko ya Mto Kalambo. Kutokana na kuwepo kwa maporomoko hayo, eneo hili lina bioanuai nyingi. Kwa kuzingatia umuhimu wa eneo hilo, mwaka 2019, Serikali ilipandisha hadhi msitu huo kwa Tangazo Na. 127 kuwa Msitu wa Mazingira Asilia.

Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS), mwaka 2016 ilianza kuboresha miundombinu katika Maporomoko ya Kalambo ili kuwezesha watalii kuvifikia kivutio husika kwa urahisi, ikiwa ni pamoja na kujenga ofisi sita, kutengeneza njia za kutembelea wageni (walk trail) na kujenga ngazi katika maporomoko ya Mto Kalambo ambapo hadi sasa takribani ngazi zenye urefu wa mita 450 zimekamilika.

Mheshimiwa Spika, aidha, kazi ya ujenzi iliyoanza mwaka 2018 ambayo inahusisha ujenzi wa jengo la ofisi, ngazi zenye urefu wa mita 514, vyoo na geti inayofanywa na kampuni iitwayo Green Construction Limited inaendelea kufanyika katika maporomoko hayo na kazi hii inatarajiwa kukamilika ndani ya mwaka huu wa 2020.

Mheshimiwa Spika, ili kuboresha mazingira ya utalii katika eneo hilo, Serikali itahamasisha sekta binafsi ili zijengwe nyumba za kulala wageni, kumbi za mikutano na eneo la kuhifadhi wanyamapori hai (zoo) ili kuweka mazingira rafiki kwa watalii.