Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 19 Sitting 2 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 13 2020-04-01

Name

Mussa Bakari Mbarouk

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Tanga Mjini

Primary Question

MHE. MUSSA B. MBAROUK aliuliza:

Tarehe 12 Septemba, 2019 katika Mkutano wa Kumi na Sita wa Bunge yamepitishwa Marekebisho ya Sheria ya Utumishi wa Umma ili kumpa Katibu Mkuu Kiongozi Mamlaka ya mwisho ya uhamisho wa watumishi wa umma.

Je, kwa kumpa Mamlaka ya Mwisho Katibu Mkuu Kiongozi hakutasababisha ukiritimba katika uhamisho wa Watumishi wa Umma?

Name

Capt. (Mst). George Huruma Mkuchika

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Newala Mjini

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, ninapenda kujibu swali la Mheshimiwa Mussa Bakari Mbarouk, Mbunge wa Tanga Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Utumishi wa Umma Sura 298, imefanyiwa marekebisho katika Kifungu cha 4(3) kupitia Kifungu cha 69 cha Sheria ya Marekebisho ya Sheria Mbalimbali Na. 13 ya Mwaka 2019 kwa kumpa Katibu Mkuu Kiongozi Mamlaka ya Mwisho ya Uhamisho wa Watumishi wa Umma kwa kuzingatia Mamlaka yake kama Mkuu wa Utumishi wa Umma kwa mujibu wa Kifungu cha 4(2) cha Sheria hii.

Mheshimiwa Spika, pamoja na Mamlaka hayo, Kifungu cha 8(2) cha Sheria hiyo kinampa Katibu Mkuu (Utumishi) Mamlaka ya kuwa Msaidizi Mkuu wa Katibu Mkuu Kiongozi. Hivyo, katika kutekeleza majukumu ya Katibu Mkuu Kiongozi, Kifungu cha 8(3)(h) cha Sheria husika kinampa Katibu Mkuu (Utumishi) Mamlaka ya kuhamisha Watumishi wa Umma kutoka Taasisi moja kwenda nyingine Tanzania Bara.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, ili kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi, Katibu Mkuu (Utumishi) amekasimu Mamlaka yake kwa Katibu Mkuu (TAMISEMI) ili aweze kuhamisha Watumishi wa Umma katika Mamlaka za Serikali za Mitaa. Vilevile, Katibu Mkuu (Utumishi) amekasimu Mamlaka yake kwa Makatibu Tawala wa Mikoa ili waweze kuhamisha Watumishi wa Mamlaka za Serikali za Mitaa katika Mikoa yao. Pamoja na kukasimisha Mamlaka yake, Katibu Mkuu (Utumishi) anaweza kuhamisha Watumishi katika Mamlaka za Serikali za Mitaa yeye mwenyewe pale inapobidi.

Mheshimiwa Spika, Ninapenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kuwa marekebisho yaliyofanyika katika Sheria ya Utumishi wa Umma Sura 298, yamempa Katibu Mkuu Kiongozi Mamlaka ya mwisho ya uhamisho wa Watumishi wa Umma ili kuwezesha uhamisho unaofanywa naye kutopingwa au kutotenguliwa na Mamlaka nyingine. Hata hivyo, Mamlaka hayo yatatumika kwa kuzingatia masilahi mapana katika Utumishi wa Umma au pale ambapo Katibu Mkuu Kiongozi hakuridhika na uhamisho uliofanywa na Mamlaka nyingine zilizopewa au zilizokasimiwa madaraka hayo kama ilivyoelezwa.