Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 52 Public Service Management Ofisi ya Rais (Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora) 450 2019-06-25

Name

Anatropia Lwehikila Theonest

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANATROPIA L. THEONEST Aliuliza:-

Je, ni likizo ya muda gani wamekuwa wakipewa wazazi (watumishi wanawake na wanaume) pale wanapopata watoto mapacha zaidi ya wawili au watoto njiti?

Name

Dr. Mary Machuche Mwanjelwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mbeya Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Anatropia Lwehikila Theonest, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni H. 12(2) ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za Mwaka 2009, mtumishi wa umma mwanamke anapojifungua mtoto hupewa likizo ya uzazi ya muda wa siku 84 mara moja kila baada ya miaka mitatu. Hata hivyo, kwa mujibu wa Kanuni H. 12(3) ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009, mtumishi husika anapojifungua watoto zaidi ya mmoja hupewa siku 14 zaidi za likizo ya uzazi na hivyo kuweza kuwa siku 98. Kanuni tajwa haikubanisha muda wa likizo ya uzazi kwa mtumishi anayejifungua mtoto njiti.

Mheshimiwa Spika, matukio ya uzazi wa mapacha zaidi ya wawili (triple) na watoto njiti ni nadra kutokea mara kwa mara. Hivyo, Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009 hazikuainisha masharti ya likizo ya uzazi kwa matukio kama hayo. Hivyo, natoa wito kwa waajiiri na wasimamizi wa rasilimaliwatu katika utumishi wa umma kutoa taarifa kwa Katibu Mkuu wa Utumishi na kuomba kibali cha kuongezewa muda wa likizo ya uzazi kwa watumishi wa umma walio chini yao pindi wanapojifungua watoto mapacha zaidi ya wawili au watoto njiti.

Mheshimiwa Spika, kwa mujibu wa Kanuni H.13 ya Kanuni za Kudumu katika Utumishi wa Umma za mwaka 2009, Mtumishi wa Umma mwanaume hupewa likizo ya uzazi ya angalau siku tano kuanzia siku ya kuzaliwa mtoto ili aweze kuhudumia familia yake. Hata hivyo, iwapo kuna sababu za msingi zinazomlazimisha kuendelea kuhudumia familia kwa ukaribu, mtumishi husika anaweza kuomba ridhaa kwa mwajiri wake ya kuongezewa ili siku kadhaa kuhudumia familia.

Mheshimiwa Spika, hivyo, inapotokea mtumishi wa umma kajifungua watoto mapacha zaidi ya wawili au watoto njiti na kulazimika kuwa na muda wa zaidi wa kuhudumia watoto hao, mwajiri wake anapaswa kuwasilisha hoja kwa Katibu Mkuu (Utumishi) ilia toe kibali cha kuongeza muda wa likizo ya uzazi. Ahsante.