Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 51 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 443 2019-06-24

Name

Daimu Iddi Mpakate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kusini

Primary Question

MHE. DAIMU I. MPAKATE aliuliza:-

Kituo cha Polisi Lukumbule kiliungua moto miaka iliyopita na mpaka sasa kituo hicho hakina Askari kimefungwa:-

(a) Je, ni lini Serikali itakirejesha kituo hicho hasa ikizingatiwa kuwa kipo mpakani mwa nchi ya Msumbiji?

(b) Je, ni lini Serikali itaweka kituo cha Uhamiaji katika kituo hicho cha Lukumbule?

(c) Je, Serikali ina mpango gani wa kumalizia ujenzi wa Kituo cha Polisi Lukumbule ambacho kimeishia kwenye lenta baada ya Halmashauri kushindwa kumalizia ujenzi huo?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi napenda kujibu swali la Mheshimiwa Daimu Idd Mpakate, Mbunge wa Tunduru Kusini, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Kituo cha Polisi Lukumbule kilichomwa moto mwaka 2013 na baadhi ya wananchi wasiotaka kutii sheria katika eneo hilo. Baada ya tukio hilo Jeshi la Polisi kwa kutambua kwamba eneo husika ni la mpakani na nchi ya Msumbiji limekuwa likifanya doria za mara kwa mara na pia kushirikisha taasisi nyingine za Serikali ambazo ni wadau wa ulinzi na usalama katika kuimarisha hali ya ulinzi na usalama kwa wananchi wa eneo hilo.

Mheshimiwa Naibu Spika, mpango wa kufungua Kituo cha Uhamiaji Kata ya Lukumbule upo kwenye hatua za mwisho na inatarajiwa kufanguliwa wakati wowote mwaka ujao wa fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuupongeza uongozi wa Halmashauri ya Tunduru kwa ujenzi wa kituo cha Polisi cha Lukumbule ingawa bado ujenzi wake haujakamilika. Hata hivyo, Serikali inatambua umuhimu na uhitaji wa kituo cha Polisi katika eneo hilo. Aidha Serikali kupitia Jeshi la Polisi itafanya tathmini ili kubaini gharama halisi za kukamilisha sehemu ya ujenzi uliobakia na kuona uwezekano wa kukamilisha ujenzi huo.