Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 15 Information, Culture, Arts and Sports Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo 123 2016-05-09

Name

Martha Jachi Umbulla

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FLATEI G. MASSAY (K.n.y. MHE. MARTHA J. UMBULLA) aliuliza:-
Ujenzi wa senta ya Michezo ya riadha katika Mkoa wa Manyara hususani Wilaya ya Mbulu imekuwa ni kilio cha muda mrefu kwa viongozi na wananchi wa eneo husika kutokana na vijana wengi kuwa na vipaji katika mchezo wa riadha na michezo mingine:-
(a) Je, ni lini Serikali itasikiliza kilio cha muda mrefu na kujenga senta ya michezo ya riadha Mkoani Manyara ili vijana wengi wenye vipaji waweze kunufaika?
(b) Je, Serikali haioni kuwa kwa kujenga senta ya michezo Manyara itaweza kupunguza changamoto ya ukosefu wa ajira kwa vijana wa Mkoa huo na maeneo jirani kama Singida, Arusha na Dodoma ambako kuna vipaji hivyo?

Name

Nape Moses Nnauye

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mtama

Answer

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mkoa wa Manyara na Wilaya zake una vijana wenye vipaji vya riadha na michezo mingine. Aidha, Serikali inatambua pia umuhimu wa kuwa na kituo kikubwa cha michezo hasa ya riadha ambacho pamoja na mambo mengine kitasaidia kuibua, kukuza na kuviendeleza vipaji vya vijana ikiwa ni pamoja na kuwapatia ajira vijana mkoani humo.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo hayo ya utangulizi, sasa naomba kujibu swali la Mheshimiwa Massay, kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali ya Mkoa wa Manyara imepanga kujenga kituo cha michezo cha mkoa mara baada ya kukamilisha mazungumzo na kukubaliana na wananchi wanaomiliki ardhi katika eneo ambalo mkoa wamekubaliana. Aidha, kwa kipindi hiki ambacho uongozi wa mkoa hauna kituo cha michezo, mkoa umepanga kutumia kambi ya michezo ya Hifadhi ya Taifa ya Tarangire kwa muda, wakati wanasubiri kupatikana kwa eneo la kudumu la mkoa. Hii ni kutokana na sababu kuwa Hifadhi ya Taifa ya Tarangire ina hosteli na viwanja vya michezo vya kutosha.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kujengwa kwa kituo hiki katika mkoa kutaongeza ajira, kutapanua shughuli za kibiashara na hata kukua kwa uchumi wa Mkoa wa Manyara. Serikali inaendelea na mazungumzo na wananchi wamiliki wa eneo husika, yakikamilika na pesa zikipatikana ujenzi wa kituo hiki cha michezo utaanza.