Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 42 Energy and Minerals Wizara ya Nishati 349 2019-06-10

Name

Justin Joseph Monko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Singida Kaskazini

Primary Question

MHE. JUSTIN J. MONKO aliuliza:-

Jimbo la Singida Kaskazini limepata Mradi wa Umeme Vijiji (REA na BTIP) ambapo utapeleka umeme katika vijiji 54 kati ya 84; katika baadhi ya maeneo ambayo mradi umepita umeacha nyumba za wananchi, taasisi za dini, taasisi za Serikali na pampu za maji pasipo kuziunganishia umeme.

(a) Je, Serikali ina kauli gani kwa maeneo hayo yaliyorukwa na wananchi waliokwishafanya wiring kwa matarajio ya kuunanishiwa umeme?

(b) Je, ni lini Serikali itapeleka umeme katika vijiji 30 vilivyosalia?

(c) Je, Serikali ipo tayari kusaidia njia mbadala ya umeme wa jua (solar power) katika maeneo ya huduma muhimu kama zahanati, sekondari na huduma za maji wakati tukisubiri usambazaji katika vijiji vilivyosalia?

Name

Subira Khamis Mgalu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Justin Joseph Monko, Mbunge wa Singida Kaskazini lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Spika, Serikali kupitia Wakala wa Nishaji Vijijini (REA) inaendelea kupeleka umeme vijijini kwa awamu kulingana na upatikanaji wa fedha. Lengo la mradi huu ni kuhakikisha umeme katika vijiji, taasisi, viwanda na miradi ya maji na maeneo yaliorukwa katika Jimbo la Singida Kaskazini zikiwemo nyumba za wananchi, taasisi za dini, taasisi za Serikali na pampu za maji zitapelekewa umeme kupitia mradi wa REA III mzunguko wa kwanza unaoendelea na kupitia Mradi wa Densification II utakaoanza kutekelezwa mwezi Juni, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2020.

(b) Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutekeleza miradi ya kusambaza umeme vijijini ambapo vijiji 30 vilivyosalia katika Jimbo hilo vitapatiwa umeme katika mzunguko wa pili wa mradi wa REA III utakaoanza kutekelezwa kuanzia mwezi Julai, 2019 na kukamilika mwezi Juni, 2021.

(c) Mheshimiwa Spika, mwaka 2018/2019 Serikali kupitia Mradi wa Results Based Finance unaotekelezwa na Wakala wa Nishati Vijijini (REA) iliendelea kufanya utafiti ya kujua kiasi cha nguvu ya jua kinachopatikana nchini ikiwa ni pamoja na eneo la Singida Kaskazini.

Mheshimiwa Spika, baada ya kukamilika kwa utafiti huo Serikali itaanza kazi ya kupeleka miundombinu ya umeme wa nguvu za jua katika Jimbo la Singida Kaskazini. Nakushukuru. (Makofi)