Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 40 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 335 2019-05-31

Name

Pascal Yohana Haonga

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Mbozi

Primary Question

MHE. PASCAL Y. HAONGA aliuliza:-

Wilaya ya Mbozi ina vivutio vingi sana vya utalii, baadhi yake ni Kimondo kilichopo Kijiji cha Ndolezi Kata ya Mlangali, Majimoto na Mapango ya Popo katika Kata ya Nanyara, lakini baadhi ya vivutio hivyo hasa Majimoto na Mapango ya Popo havitambuliwi na havipo hata kwenye orodha ya kumbukumbu za Serikali:-

(a) Je, ni lini Serikali itavitambua rasmi vivutio hivyo?

(b) Je, kivutio cha Kimondo kimeingiza shilingi ngapi kwenye Halmashauri ya Mbozi na Serikali Kuu tangu kigunduliwe?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Pascal Yohana Haonga, Mbunge wa Mbozi lenye sehemu (a) na (b) kwa pamoja kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inavitambua vivutio vilivyopo Mkoani Songwe ikiwemo vinavyopatikana Wilaya ya Mbozi vya Majimoto na Mapango ya Popo na tayari vimeorodheshwa katika kumbukumbu za Serikali. Vivutio hivyo vilitambuliwa rasmi katika maadhimisho ya siku ya Kimondo Duniani yaliyofanyika katika Kituo cha Kimondo cha Mbozi kilichopo Kijiji cha Ndolezi, Kata ya Mlangali tarehe 28 - 30 Juni, 2018.

Mheshimiwa Spika, napenda kumjulisha Mheshimiwa Mbunge kuwa Serikali itaendelea kufanya utafiti wa kina kwa lengo la kukusanya taarifa sahihi na vivutio vilivyopo Mkoani Songwe kwa lengo la kuvitangaza katika gazeti la Serikali. Vivutio vitakavyokidhi vigezo kuwa urithi wa utamaduni wa Taifa tutavitumia kiutalii.

Mheshimiwa Spika, kuanzia Mwaka wa Fedha 2013/ 2014 hadi 2017/2018 Serikali imekusanya kiasi cha shilingi milioni 14,378,000/= kutoka katika kituo cha Mbozi kutokana na watalii waliokwenda kuona Kimondo. Kwa kutambua umuhimu wa kituo hicho, Serikali inaendelea kukiboresha kwa kujenga Kituo cha Kumbukumbu na Taarifa na kuandaa maadhimisho ya Siku ya Kimondo Duniani. Aidha, jitihada za kukitangaza kituo hicho zitaongeza idadi ya watalii ndani na nje ya nchi na hatimaye kuongeza mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)