Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 39 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 326 2019-05-30

Name

Zainab Mndolwa Amir

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAINAB M. AMIR aliuliza:-

Wananchi wengi wamejenga makazi yao bila kuzingatia mipangomiji na matokeo yake kuvunjwa nyumba zao bila kupata fidia pindi Serikali inapoanza ujenzi unaozingatia mipangomiji:-.

Je, Serikali ina mkakati gani wa kuwapatia wananchi elimu stahiki ili waepukane na adha hiyo?

Name

William Vangimembe Lukuvi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ismani

Answer

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Zainab Mndolwa Amiri, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitekeleza mikakati mbalimbali ya kuwaelimisha wananchi kuhusu ujenzi unaozingatia mipangomiji ili kuepuka madhara mbalimbali ikiwemo kubomolewa nyumba zao bila kulipwa fidia. Mikakati hiyo ni pamoja na kutoa elimu kwa njia ya vyombo vya habari kama vile redio, luninga, magazeti, vipeperushi, machapisho mbalimbali, mitandao ya kijamii pamoja na tovuti ya Wizara.

Mheshimiwa Spika, sambamba na utoaji wa elimu kupitia vyombo vya habari, viongozi wa Wizara wamekuwa wakitumia mikutano ya hadhara katika ziara zao nchini kutoa elimu kuhusu umuhimu wa wananchi kujenga kwa kufuata utaratibu hususan katika maeneo ambayo yametangazwa kuwa ni maeneo ya kimipangomiji. Aidha, kupitia kaulimbiu ya ‘funguka kwa Waziri wa Ardhi’ Mheshimiwa Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na mambo mengine amekuwa akipokea changamoto mbalimbali kuhusu ujenzi holela mijini na kutoa elimu stahiki kwa wananchi kuhusu umuhimu wa kujenga kwa kufuata utaratibu uliowekwa kwa mujibu wa sheria.

Mheshimiwa Spika, kwa maeneo ambayo yameendelezwa bila kupangwa, Serikali imetoa fursa kwa wananchi kurasimishiwa makazi yao na kupatiwa hatimiliki. Urasimishaji makazi pamoja na mambo mengine unasaidia kuwapatia wananchi fursa ya kutumia ardhi yao kama mtaji, kutoa miundombinu ya msingi, kupunguza migogoro, kuvutia uwekezaji na kuweka huduma za kijamii. Katika maeneo mengine ambayo urasimishaji haufanyiki, utambuzi wa milki na uhakiki hufanyika na wananchi wa maeneo hayo kupewa leseni za makazi ambazo zinasaidia kuimarisha usalama wa milki na kutumika kama dhamana za mikopo kutoka katika taasisi za kifedha.

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea kusisitiza kuwa wananchi wazingatie sheria na taratibu za uendelezaji miji ili kujiepusha na ujenzi holela. Aidha, wananchi waepuke kujenga mijini bila kuwa na vibali vya ujenzi ili kuepuka maafa na madhara kwa mali zao.