Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 39 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 325 2019-05-30

Name

Ruth Hiyob Mollel

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DKT. IMMACULATE S. SEMESI (K.n.y. MHE. RUTH H. MOLLEL) aliuliza:-

Migogoro ya wakulima na wafugaji imekuwa tatizo sugu katika maeneo mengi nchini pamoja na kazi kubwa ambayo imefanywa na Serikali:-

(a) Je, Serikali imetenga kiasi gani cha bajeti kwa ajili ya kupanga matumizi ya ardhi nchi nzima?

(b) Kijiji cha Matenzi Kata ya Beta Wilayani Mkuranga kina wafugaji takribani 10,000: Je, Serikali ina mkakati gani wa kupima eneo hilo kabla migogoro haijaanza?

Name

William Vangimembe Lukuvi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ismani

Answer

WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ruth Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi kwa mujibu wa Sheria ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi Na. 6 ya mwaka 2007, ni jukumu la mamlaka ya upangaji ambazo ni Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi kwa ngazi ya Taifa na Halmashauri za Wilaya na Vijiji kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, Serikali imekuwa ikitenga fedha za kuwezesha uandaaji wa mipango ya matumizi ya ardhi kila mwaka. Katika kipindi cha mwaka wa fedha 2017/2018 hadi 2019/2020 Serikali imetenga shilingi bilioni saba za matumizi ya kawaida na maendeleo kwa ajili ya kupanga matumizi ya ardhi na kutatua migogoro ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Spika, kwa mwaka 2018/2019 Serikali kupitia Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi, iliendelea kuwezesha upangaji wa matumizi ya ardhi katika vijiji vyote vinavyozungukwa na hifadhi za misitu na hifadhi za Taifa. Kazi hii itaendelea katika mwaka wa fedha 2019/ 2020 ikijumuisha upangaji wa matumizi ya ardhi katika vijiji vyote vinavyopitiwa na Mradi wa Bomba la Mafuta pamoja na wilaya zote mpakani mwa nchi jirani. Aidha, wadau mbalimbali wa maendeleo wamekuwa wakiwezesha mamlaka za upangaji kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi katika maeneo mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Spika, Sheria ya Uandaaji wa Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi Na. 6 ya mwaka 2007, kifungu cha 33(1) kinatoa mamlaka kwa Halmashauri za vijiji kujiandalia mipango ya matumizi ya ardhi. Vilevile, vifungu vya 9(1) na 21(2)(b) vya Sheria ya Ardhi ya Vijiji Na. 5 ya mwaka 1999 na miongozo ya kuandaa mipango ya vijiji wa mwaka 2013 vinatoa mamlaka kwa Halamshauri za Wilaya kujengea vijiji vyake uwezo na kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi pamoja na kuratibu kazi hizo.

Mheshimiwa Spika, Tume ya Taifa ya Mipango ya Matumizi Bora ya Ardhi imeshajengea uwezo na kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi ya vijiji katika Halmashauri ya Wilaya ya Mkuranga. Hivyo, ni jukumu la Halmashauri hiyo kuendeleza kazi ya kuandaa mipango ya matumizi ya ardhi ya vijiji vyake kwa kutoa kipaumbele kwenye vijiji vyenye migogoro ya matumizi ya ardhi na tishio kwa hifadhi ya ardhi na mazingira, hususan hicho Kijiji ambacho Mheshimiwa amekitaja cha Beta ambacho anasema kina mifugo zaidi ya 10,000.