Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 38 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 321 2019-05-29

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA aliuliza:-

Katika Bajeti ya Mwaka 2017/2018 Serikali iliondoa kodi kwenye taulo za kike (pads) jambo ambalo ni muhimu sana kwa maisha ya Wanawake na Wasichana mpaka sasa ni mwaka mmoja tangu kodi hizo ziondolewe lakini bei ya taulo za kike haijashuka licha ya kuondolewa kwa kodi hizo Nchi nzima.

Je, ni lini Serikali itasimamia kwa ukamilifu suala hilo ili bei za taulo za kike zishuke na kusaidia afya za Wanawake hususani Wasichana?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Sophia Hebron Mwakagenda, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, hatua ya kuondoa kodi ya ongezeko la thamani kwenye taulo za kike ililenga kupunguza sehemu ya gharama za uzalishaji wa bidhaa hiyo na mojawapo ya athari chanya iliyotegemewa ni kushuka kwa bei ya bidhaa hiyo. Pamoja na Serikali kuchukua hatua ya kuondoa kodi imebainika kuwa hakuna mabadiliko ya bei ya bidhaa hiyo katika soko. Hii inatokana na ukweli kuwa, bei ya bidhaa katika soko inaamuliwa na nguvu ya soko pamoja na gharama nyingine za uzalishaji na uendeshaji kama vile gharama za malighafi, mishahara, uwekezaji, mifumo ya uzalishaji, teknolojia, ushindani katika soko, umeme, maji na majitaka, usambazaji, ubora wa bidhaa n.k. Hivyo basi kutokushuka kwa bei ya taulo za kike kunabainisha kwamba kodi inachangia sehemu ndogo sana katika kupanga bei ya bidhaa kama ambavyo Serikali imekuwa ikisisitiza na kutoa ufafanuzi mbele ya Bunge lako Tukufu.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa mfumo wetu wa uchumi ni mfumo wa soko huria, bei ya bidhaa huamuliwa na nguvu ya soko yaani ugavi na mahitaji ya soko. Fursa pekee iliyopo ni kuhamasisha uwekezaji mkubwa kwa kutumia teknolojia yenye gharama nafuu katika kutengeneza taulo za kike, kupunguza gharama nyingine sambamba na kuchochea ushindani wa bei katika soko na sio Serikali kuondoa kodi na kupanga bei ya bidhaa.