Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 36 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 299 2019-05-27

Name

Yussuf Salim Hussein

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Chambani

Primary Question

MHE. YUSSUF SALIM HUSSEIN aliuliza:-

Utalii wa Baharini kupitia “diving” unakua kwa kasi sana Duniani kote hali ambayo inaongeza soko la ajira katika sekta hiyo.

(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kukabiliana na changamoto za soko la ajira kwa vijana wa Kitanzania?

(b) Je, Serikali imejipanga vipi kuhakikisha usalama wa watalii wanapokuwa chini ya maji hasa kutokana na uvuvi haramu wa kutumia mabomu?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Yussuf Salim Hussein, Mbunge wa Chambani lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, utalii wa kuzamia (diving) ni moja kati ya shughuli za kitalii ambazo zinafanyika hapa Nchini katika bahari ya Hindi kwenye meeneo ya hifadhi ya bahari ya maeneo tengefu. Idadi ya watalii wanaotembelea maeneo hayo imekuwa ikiongezeka ambapo hadi hivi sasa idadi imefikia watalii 46000. Aidha, kutokana na idadi hiyo ya watalii na uwekezaji unaofanyika katika maeneo hayo, ajira nyingi zinaendelea kuzalishwa na kipato kuongezeka kwa Wananchi na Taifa kwa ujumla. Vilevile Serikali kupitia uongozi wa maeneo hayo imekuwa ukihamasisha vijana kujiunga na mafunzo ya uzamiaji na kuongoza watalii ili waweze kunufaika na ajira katika sekta husika.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa mafunzo ya utalii wa kuzamia yanatolewa katika vituo vya uzamiaji vya diving centres vinavyotambuliwa Kisheria katika maeneo ya hifadhi ya bahari ya maeneo tengefu ya Mafia vituo vinne, Dar es salaam vituo viwili na Tanga vituo viwili. Mafunzo hayo yanatolewa kwa vijana wanaoishi katika maeneo jirani na hifadhi ya bahari ya maeneo tengefu ili kuwajengea uwezo utakaowawezesha kupata ajira katika sekta husika.

Mheshimiwa Spika, utalii wa kuzamia ni taaluma ambayo hupatikana baada ya mtu kupata mfunzo ya kuzamia ambapo huambatana na mafunzo ya usalama na uokoaji. Aidha, kwa mujibu wa taratibu za Kimataifa, wazamiaji hupaswa kuwa na Bima ya Maisha ambayo husaidia kutoa fidia na matibabu endapo ataumia na kupata ajali wakati za uzamiaji.

Vilevile wazamiaji huhimizwa kutumia vifaa vyenye ubora ili kuepusha madhara yanayoweza kujitokeza wakati wa uzamiaji. Vifaa hivyo ni pamoja na Mitungi ya gesi, Boyance control device, Regulator, Mask, Fins, Wet or Dry suit, Dive computer na Snorkel na vifaa vingine muhimu.

Mheshimiwa Spika, maeneo yanayotumika kwa ajili ya shughuli za uzamiaji katika hifadhi yameainishwa na kuhakikishwa kuwa uvuvi haramu na vilipuzi havipo. Hata hivyo Serikali imeendelea na jitihada za kudhibiti uvuvi haramu ikiwemo matumizi ya vilipuzi kwa kushirikiana na wadau mbalimbali. Hadi sasa uvuvi huo umedhibitiwa kwa kiwango kikubwa katika maeneo yote ya bahari ya Hindi na hivyo kufanya maeneo hayo kuwa salama kwa watalii wanaozamia.