Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 34 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 285 2019-05-23

Name

Naghenjwa Livingstone Kaboyoka

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NAGHENJWA L. KABOYOKA aliuliza:-

Wananchi wa Jimbo la Same Mashariki wako tayari kuanzisha misitu ya vijiji kwenye maeneo yenye ukame kama vile Kata za Bendera, Kihurio, Ndugu na Maore ili kuhifadhi mazingira.

Je, Serikali ipo tayari kuanzisha miradi ya utunzaji wa mazingira katika kata tajwa kwa kufundhisha wanavijiji uanzishwaji wa misitu ya vijiji?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Naghenjwa Livingstone Kaboyoka, Mbunge wa Same Mashariki kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wilaya ya Same kiikoloji na kijiografia imegawanyika katika Kanda kuu mbili, yaani ukanda wa mlimani ambapo hali yake ya hewa ni nzuri ukilinganisha na ukanda wa tambarare ambapo hali ya hewa ni ukame. Kwa maana hiyo, kata zilizotajwa na Mheshimiwa Mbunge zipo katika ukanda wa tambarare na kwa bahati nzuri zina uoto wa misitu.

Mheshimiwa Spika, Wizara imeweka utaratibu wa kushirikiana na halmashari za wilaya na wananchi katika kutekeleza majukumu yake ya usimamizi wa maliasili. Mathalani, katika halmashauri ya Wilaya ya Same, utunzaji wa mazingira umehusisha utoaji wa elimu kwa wananchi na kuanzisha Kamati za Maliasili na Misitu, kuandaa mipango ya usimamizi na kutunga sheria ndogo za usimamizi wa maliasili. Vilevile, kupitia utaratibu huu wananchi wanashirikiana na Wizara na halmashauri kupanda miti kwenye maeneo ya wazi.

Mheshimiwa Spika, Serikali iko tayari kuendelea kutekeleza azma ya kuwasaidia wananchi wa Kata za Bendera, Kihurio, Ndungu na Maore kuhusu shabaha yao ya kutunza misitu hiyo ya asili. Hii inatokana na ukweli kwamba pamoja na kuwa vijiji hivi viko nyanda za ukame bado vina uoto mzuri wa asili ambao ukitunzwa vizuri utasaidia kuboresha hali ya hewa, uhifadhi wa baionuai na huduma za kijamii kama maji.