Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 15 Sitting 32 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 270 2019-05-21

Name

Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Primary Question

MHE. JOSEPH M. MKUNDI aliuliza:-

Visiwa vya Ukerewe bado havitumiki ipasavyo kama eneo mahsusi kiutalii ingawa vimo vivutio vingi vya utalii ikiwemo jiwe linalocheza:-

Je, Serikali ina mkakati gani wa kushirikiana na vikundi kama vile vya mila na desturi Ukerewe (KUMIDEU) katika kukitangaza Kisiwa cha Ukerewe kama eneo la utalii?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Joseph Michael Mkundi Mbunge wa Ukerewe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu inatambua kuwa Ukerewe ni miongoni mwa Visiwa vichache nchini vyenye rasilimali mbalimbali ikiwemo fukwe nzuri, utalii wa utamaduni pamoja na jiwe linalocheza. Vivutio hivi kwa miaka ya hivi karibuni vimekuwa vikivutia wageni wengi kutembelea maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Wizara inaendelea na zoezi la kuainisha vivutio vya utalii kwa dhumuni la kuviendeleza pamoja na kuvitangaza. Katika mwaka wa Fedha wa 2019/2020 tunatarajia kutekeleza zoezi hilo hilo katika Mikoa mbalimbali ikiwemo Mwanza. Kazi hiyo hutekelezwa kwa kushirikiana na Uongozi wa Mkoa, Wilaya, Vijiji na wadau wa Sekta ya Utalii katika maeneo hayo, hivyo nimjulishe Mheshimiwa Mbunge, zoezi hilo litakapoanza kutekelezwa katika Mkoa wa Mwanza, Wataalam wangu watapita katika Kisiwa cha Ukerewe ikiwa ni pamoja na kufanya kazi hiyo kwa kushirikiana na kikundi cha Mila na Desturi cha Ukerewe cha (KUMIDEU)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi hilo ni juhudi za makusudi za Wizara yangu za kupanua wigo wa mazao ya utalii kwa kubainisha vivutio vya utalii wa asili sehemu mbalimbali nchini. Aidha, kwa kutambua umuhimu wa kusimamia na kuendeleza Sekta ya Utalii Kanda ya Ziwa, Wizara ilifungua Ofisi ya Kanda iliyohusisha Idara ya Utalii na Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) katika Jiji la Mwanza. Lengo likiwa ni kusogeza kwa karibu huduma kwa wadau wa Sekta ya Utalii walio katika Kanda ya Ziwa na maeneo jirani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue fursa hii, kumpongeza Mheshimiwa Mbunge kwa jitihada zake za kuhakikisha Sekta ya Utalii inazidi kuendelea na kukua hususani katika Kisiwa cha Ukerewe na Mkoa wa Mwanza kwa ujumla. Ifahamike kwamba Sekta ya Utalii ni Mtambuka na hivyo kazi ya uendelezaji sekta hii inahitaji juhudi za pamoja za wadau wa Sekta hii, Umma na Binasfsi. Hivyo, Wizara yangu itaendelea kushirikiana kwa karibu na wadau wa Sekta ya Utalii kuendeleza utalii nchini ahsante.