Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 9 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 121 2019-09-13

Name

Lucy Simon Magereli

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. LUCY S. MAGERELI aliuliza:-

Mwaka 2018 Serikali ilipitisha Sheria ya Udhibiti ya Taasisi Ndogo za Fedha SACCOS, VICOBA, Vikundi vya kuchangishana na kukopeshana, vyote vipate usajili na kusimamiwa na Benki Kuu ya Tanzania:-

(a) Je, zoezi hili limeshatekelezwa kwa asilimia ngapi na ni taasisi ngapi zimesajiliwa?

(b) Je, Serikali haioni kuwa zoezi hili ni over – regul ation na kuwanyima fursa ambayo imekuwa ikiwasaidia wakopaji na wakopeshaji wadogo kusaidiana katika jamii zao?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango naomba kujibu swali la Mheshimiwa Lucy Simon Magereli Mbunge Viti Maalum kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lako Tukufu lilitunga Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha Mwaka 2018. Baada ya Sheria hiyo kutungwa Serikali ilianza mchakato wa kuandaa Kanuni za Huduma Ndogo za Fedha. Kanuni hizo zinalenga madaraja manne ya watoa huduma yaliyoanishwa kwenye Sheria. Aidha, mchakato huu ulihusisha ukusanyaji wa taarifa mbalimbali za walengwa ili kuweza kutengeneza kanuni zinazozingatia hali halisi ya biashara zao pamoja na matakwa ya sheria. Mchakato wa kuandaa Kanuni umekamilika na hivyo kutangazwa kwenye gazeti la Serikali Na. 575 tarehe 2 August Mwaka 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, kwa mujibu wa sheria hii, walengwa wamepewa makataa yaani grace period ya mwaka mmoja baada ya kununi kutolewa ili waweze kujiandaa kulingana na matakwa ya kanuni hizo. Kanuni zitaanza kutumika rasmi baada ya muda wa makataa kupita ikiwemo zoezi la usajili. Hivyo basi, hadi sasa hakuna taasisi yoyote iliyosajiliwa kupitia Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha ya Mwaka 2018.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, lengo la kutungwa kwa Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha siyo kunyima jamii fursa ya kusaidiana kwa njia ya kukopesha na kukopeshana, bali ililenga kutatua changamoto zilizojitokeza wakati wa utekelezaji wa Sera ya Taifa ya Huduma Ndogo za Fedha ya mwaka 2000. Changamoto hizo ni pamoja na kiwango kikubwa cha riba na ukosefu wa utaratibu wa kuwalinda walaji na wadau wa sekta ndogo ya fedha kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni matarajio ya Serikali yetu kuwa Sheria ya Huduma Ndogo za Fedha ya mwaka 2018, itaimarisha usimamizi na udhibiti wa sekta ya huduma ndogo za fedha na hivyo kuakisi matarajio na mahitaji ya wadau, kasi ya ukuaji na mchango wake katika sekta nzima ya fedha na uchumi wa taifa letu kwa ujumla.