Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 9 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 114 2019-09-13

Name

Najma Murtaza Giga

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ASHA ABDULLAH JUMA (K.n.y. MHE. NAJMA MURTAZA GIGA) aliuliza:-

Utaratibu wa kuweka pamoja watuhumiwa wenye makosa tofauti kama vile, wizi wa kuku, mazao, mauaji, ujambazi sugu na ubakaji ni utaratibu wa kawaida katika magereza na mahabusu zetu hapa nchini, hali kadhalika kwa wafungwa wenye rika tofauti:-

(a) Je, Serikali haioni kuwaweka pamoja wafungwa na watuhumiwa hao ni hali hatarishi kwa mustakabali wa maisha yao ya baadae?

(b) Je, Serikali haioni inapoteza nguvu kazi ya vijana wetu kwa kuwachanganya pamoja na wale wabakaji hususan vijana wa kuanzia umri wa miaka 18 hadi 30?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Najma Murtaza Giga, Mbunge wa Viti Maalum, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya jukumu la Jeshi la Magereza ni kuwapokea na kuwahifadhi magerezani wahalifu wa aina zote wanaoletwa kwa mujibu wa Sheria, Kanuni na Taratibu za nchi. Sanjari na jukumu hilo, Kanuni za Uendeshaji wa Magereza za mwaka 1967 (The Prisons Management Regulations) zinaelekeza kuwa uhifadhi wa wahalifu magerezani utafanyika kwa kuzingatia utenganisho kwa vigezo vya jinsia, umri, kosa na kifungo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kuwa katika baadhi ya magereza yetu nchini hususani magereza yenye mahabusu, suala la kuwatenganisha wahalifu kwa kuzingatia vigezo vya umri, kosa na kifungo limekuwa halizingatiwi kutokana na sababu ya msongamano wa mahabusu na uhaba wa mabweni na hivyo kupelekea mahabusu kuchanganywa na wafungwa. Hata hivyo, katika kukabiliana na hali hiyo, Serikali imeshachukua hatua mbalimbali ikiwemo kujenga magereza katika Wilaya zisizokuwa na magereza, kufanya upanuzi na kujenga mabweni kwenye magereza na kutoa elimu kwa wahalifu juu ya madhara hasi ya vitendo ya uhalifu katika jamii na kutojihusisha na vitendo hivyo katika maisha yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda ilieleweke kwamba kitendo cha wahalifu wa aina mbalimbali kuwemo magerezani au kuchanganywa hakuhalalishi wao kuendelea na vitendo vyao vya uhalifu kwani zipo Sheria, Kanuni na Taratibu za Magereza ambazo zinakataza na zinatoa adhabu kwa mhalifu endapo atabainika kufanya vitendo hivyo akiwa gerezani. Mathalani Kanuni ya makosa Gerezani ya Mwaka 1967 (The Prison Offences Regulations).

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kanuni hii imeainisha makosa mbalimbali ambayo mhalifu hapaswi kuyafanya akiwa gerezani sanjari na hatua za kuchukua na adhabu endapo itabainika ametenda kinyume. Hivyo msingi wa kanuni hii ni kuwataka wahalifu watambue kuwa wanapaswa wajirekebishe kwa kuachana na tabia ya kufanya vitendo vya kihalifu na pia Serikali inathamini na kulinda nguvu kazi yao.