Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 9 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 110 2019-09-13

Name

Martha Jachi Umbulla

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MARTHA J. UMBULLA aliuliza:-

Mwaka 2012 Mahakama ilitoa hukumu kuwa wakulima na wafugaji wote waondoke ndani ya Hifadhi ya Jamii ya Emborley Murtangos iliyoko Wilayani Kiteto lakini baadhi ya wananchi walipinga amri hiyo na kuendelea kufanya shughuli zao na kusababisha mgogoro baina ya wakulima na wafugaji:-

(a) Je, Serikali imeshughulikia kwa kiasi gani mgogoro huo uliodumu kwa miaka 8?

(b) Je, Serikali ilichukua hatua gani kuwadhibiti na kuwaadhibu waliokiuka amri hiyo?

(b) Je, nini kauli ya Serikali juu ya matumizi ya Hifadhi hiyo ili kumaliza mgogoro huo?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kibali chako, naomba kabla ya kujibu swali la msingi la Mheshimiwa Mbunge, uniruhusu niwapongeze na kuwashukuru sana Kamati za Mitihani ya Darasa la Saba ngazi ya wilaya na mikoa, walimu wetu, wanafunzi, wazazi na wadau wote wa elimu Tanzania kwa juzi na jana kumaliza zoezi la mitihani ya darasa la saba. Taarifa njema ni kwamba mitihani hiyo imetoka salama hakuna mtihani uliovuja. Tnawashukuru sana Kamati na hasa Baraza la Mitihani, Wizara ya Elimu na TAMISEMI. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais – TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Martha Jachi Umbulla, Mbunge wa Viti Maalum lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2014/2015, Serikali iliunda Kikosi Kazi cha wataalamu kutoka Ofisi ya Rais - TAMISEMI, Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Wizara ya Mipango na Fedha (Ofisi ya Taifa ya Takwimu), Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Manyara na Halmashauri ya Wilaya ya Kiteto kwa lengo la kuhakiki mipaka ya hifadhi, kupima na kuweka alama za mipaka na kuandaa mpango wa matumizi ya ardhi kwenye vijiji vinavyozunguka hifadhi hiyo. Baada ya kufanyika kwa kazi hiyo, eneo la hifadhi lilibaki na ukubwa wa hekta 75,394.6 kutoka hekta 133,333 za awali na kusajiliwa kwa namba 79667.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imeendelea kuwaondoa wananchi wa makundi ya wakulima na wafugaji wanaondelea kuingia kwenye hifadhi. Kuanzia mwaka 2014-2019, wananchi 49 wamefikishwa mahakamani kwa kukiuka amri ya Mahakama na makubaliano ya matumizi ya ardhi yaliyoidhinishwa.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la Hifadhi ya Emborley Murtangos litabaki kuwa eneo la hifadhi ya jamii kwa kuzingatia mpango wa matumizi bora ya ardhi kama ilivyoidhinishwa na kwa kuzingatia maamuzi ya Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufaa. Aidha, hali ya ulinzi na usalama katika eneo hilo itaendelea kuimarishwa ili kuhakikisha panakuwepo na amani na utulivu wakati wote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazielekeza Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa na Wilaya kuchukua hatua stahiki pale inapobainika ukiukwaji wa matumizi ya ardhi kwenye eneo la hifadhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante.