Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 7 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 95 2019-09-11

Name

Boniphace Mwita Getere

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bunda

Primary Question

MHE. BONIPHACE M. GETERE Aliuliza:-

Idadi ya watu nchini inaongezeka kwa kasi sana na watu wanahitaji maendeleo; aidha ukuaji huu una matokeo hasi na chanya:-

Je, Serikali ina mikakati gani ya kutumia au kudhibiti kasi ya idadi ya watu?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Boniphace Mwita Getere, Mbunge wa Bunda Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, utafiti wa idadi ya watu duniani unaonyesha kwamba idadi kubwa ya watu ni fursa kwa nchi iwapo baadhi ya mambo matano yatafanyika:-

(i) Kuboresha maisha ya watoto na kuboresha elimu na uwezeshaji kwa wanawake;

(ii) Kuimarisha uwekezaji katika afya ili kuwa na nguvukazi bora na yenye tija;

(iii) Kuimarisha uwekezaji katika elimu ya juu ili kuwa na nguvukazi yenye elimu, ujuzi na ubinifu;

(iv) Mageuzi ya kiuchumi yanayolenga kuharakisha ukuaji wa uchumi na upatikanaji wa kazi kwa ajili ya nguvukazi iliyopo; na

(v) Mageuzi ya Sera ili kuvutia uwekezaji wa kigeni na kuhakikisha uwajibikaji hasa katika rasilimali za umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dhima ya Mpango wetu wa Pili wa Maendeleo wa Miaka Mitano 2016/2017 – 2020/2021 ni kujenga uchumi wa viwanda ili kufungamanisha ukuaji wa uchumi na maendeleo ya watu. Mpango huu wa Pili umejikita zaidi katika uwekezaji wa kimkakati katika Sekta ya Viwanda kuimarisha miundombinu ya usafiri na usafirishaji, kusambaza umeme mijini na vijijini, kusambaza pembejeo za kilimo kwa wakati, kutatua changamoto ya muda mrefu ya upatikanaji wa umeme wa uhakika kwa kujenga bwawa kubwa la kufua umeme katika Mto Rufiji na kuimarisha huduma za jamii kwa kujenga na kukarabati miundombinu ya maji, hospitali na Vituo vya Afya vya Umma, shule pamoja na kutekeleza kwa ufanisi Sera ya Elimu Bila Malipo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, miradi inayoendelea kutekelezwa na Serikali ya Awamu ya Tano inalenga kufungamanisha fursa za kiuchumi na ongezeko la idadi ya watu; na jitihada hizi zinalandana na mambo yaliyopendekezwa kwenye ripoti ya utafiti ya idadi ya watu duniani na athari zake. Hata hivyo, matokeo chanya yataonekana kama kila Mtanzania atashiriki kikamilifu katika uzalishaji mali na huduma za jamii kuanzia ngazi ya kaya hadi Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo jambo baya kudhibiti ongezeko la idadi ya watu kama familia au Taifa limefikia kiwango cha mwisho cha kutumia rasilimali (optimal utilization) ya rasilimali zake za asili pamoja na mikakati mingine mbadala. Hata hivyo, Taifa letu bado lina rasilimali asili za kutosha kama vile ardhi ya kulima, bahari, maziwa, mito na mabonde, madini, misitu, jiografia ya usafiri na usafirishaji pamoja na fursa za utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni jukumu letu kama Taifa kuanzia ngazi ya kaya kuakisi jitihada zinazofanywa na Serikali yetu na hatimaye kutumia fursa hizi kwa ufanisi kwa lengo la kuongeza kasi ya uzalishaji mali pamoja na kuongeza kasi ya kupunguza umasikini badala ya kuogopa ongezeko la idadi ya watu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba kwa sasa Serikali imejielekeza zaidi katika kuweka mazingira wezeshi ya uwekezaji na kufanya biashara na hivyo kutumia ongezeko la idadi ya watu kama fursa ya nguvukazi ya kuzalisha mali pamoja na soko la bidhaa na huduma.