Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 7 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 85 2019-09-11

Name

Richard Phillip Mbogo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nsimbo

Primary Question

MHE. RICHARD P. MBOGO Aliuliza:-

Mabadiliko ya Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa Sura 290 yameleta nafuu sana kwa wakulima, lakini wakati huo huo Halmashauri za Wilaya zenye wakulima zenye wakulima wadogo zimeathirika kimapato na kusababisha kushindwa kutatua kero za wananchi kwa wakati:-

(a) Je, Serikali inaweza kuangalia upya suala la utoaji Ruzuku za maendeleo?

(b) Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo imeathirika kiwango kikubwa: Je, Serikali ipo tayari kuipatia ruzuku ili kutoa huduma za Elimu na Afya?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITAIRA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa ruhusa yako kabla ya kujibu swali la Mheshimiwa Richard Mbogo, naomba uniruhusu niwatakie heri vijana wetu, watoto wetu wa Darasa la Saba ambao leo na kesho wanafanya mitihani yao ya kumaliza Darasa la Saba na wanafunzi hao wapo takribani 947,221 wa kawaida na wale wenye mahitaji maalumu.

Nawaomba watu wote ambao wanahusika na zoezi hili la mitihani, wazingatie taratibu na kanuni na miongozo na kamwe wasijihusishe na udanganyifu kwa namna yoyote ile ili matokeo yawe yawe mazuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba sasa kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI nijibu swali la Mheshimiwa Richard Mbogo, Mbunge wa Nsimbo, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli Serikali ilifanya mabadiliko ya Sheria ya Fedha ya Serikali za Mitaa Sura 290 kwa kuondoa kodi ambazo zilikuwa ni kero hasa kwa wakulima wadogo. Takwimu za jumla zinaonesha makusanyo ya Mamlaka ya Serikali za Mitaa yamekuwa yakiongezeka kila mwaka. Mwaka wa fedha 2016/2017 Halmashauri zilipanga kukusanya shilingi bilioni 665.4 na zikakusanya shilingi bilioni 544.8; mwaka wa fedha 2017/2018 Halmashauri zilipanga kukusanya shilingi milioni 687.3 na zikakusanya kiasi cha shilingi bilioni 553.4.

Mheshimiwa Mwenyekiti, samahani hizi zisomeke bilioni, siyo milioni. Mwaka wa fedha 2018/2019 Halmashauri zilipanga kukusanya shilingi bilioni 723.7 na zimekusanya shilingi bilioni 661.36. Hivyo, kwa tathmini ya jumla, inaonesha kuwa uamuzi wa kuondoa kodi kero haujaathiri ukusanyaji wa mapato kwenye Mamlaka za Serikali za Mitaa.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye sekta ya afya katika kipindi cha Mwaka 2017/2018 na 2018/2019, Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo shilingi bilioni moja kwa ajili ya ujenzi wa Vituo vya Afya vya Kamoge na Katumba na shilingi milioni 220 kwa ajili ya ununuzi wa vifaatiba. Vilevile katika mwaka wa fedha 2019/2020, Serikali imetenga kiasi cha shilingi milioni 500 kwa ajili ya kuanza ujenzi wa Hospitali ya Wilaya ya Nsimbo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa sekta ya elimu, mwaka wa Fedha 2018/2019, Serikali imeipelekea Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kiasi cha shilingi milioni 250 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya madarasa 20 ya shule za sekondari. Vilevile katika Mwaka wa Fedha 2018/2019 kupitia Programu ya EP4R Serikali imeipatia Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kiasi cha shilingi milioni 205.7 kwa ajili ya ujenzi wa madarasa manne, ukamilishaji ma maboma ya madarasa saba na ujenzi wa matundu ya vyoo 12 katika shule za msingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kupitia EP4R, Serikali imeipatia Halmashauri ya Nsimbo kiasi cha shilingi milioni 100.6 kwa ajili ya ujenzi wa maabara na matundu sita ya vyoo shule za sekondari. Aidha, kwa Mwaka wa Fedha 2019/2020, Serikali imeitengea Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo kiasi cha shilingi milioni 421 kwa ajili ya elimu msingi bila malipo.Ahsante.