Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 6 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 74 2019-09-10

Name

Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Primary Question

MHE. ORAN M. NJEZA Aliuliza:-

Ili kuboresha kilimo na ujasiriamali inahitajika elimu kwa wakulima ikiwa ni pamoja na kuwa na vyanzo vya uhakika vya mtaji.

(a) Je, Benki ya Kilimo ina mtaji kiasi gani?

(b) Je, Benki ya Kilimo ina mkakati gani wa kuwafikia wakulima wadogo wa Wilaya ya Mbeya?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO Alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Oran Manase Njeza, Mbunge wa Mbeya Vijijini, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania ilipatiwa mtaji wa shilingi bilioni 60 mwezi Novemba, 2014. Aidha, tangu ilipoanza rasmi shughuli zake mwaka 2015, Benki ya Maendeleo ya Kilimo imefanikiwa kujiendesha na kukuza mtaji wake hadi kufikia shilingi bilioni 67.5 zilizorekodiwa mwishoni mwa robo ya kwanza ya mwaka 2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuhakikisha kuwa Benki ya Maendeleo ya Kilimo inakuwa na fedha za kutosha kwa ajili ya kutoa mikopo na hivyo kufikia malengo ya kuanzishwa kwake, Serikali imeipatia benki hii kiasi cha shilingi bilioni 103 kupitia mkopo wa gharama nafuu kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika. Aidha, kwa sasa benki inaendelea na mchakato wa kukamilisha masharti ya kupatiwa awamu ya pili ya mkopo wa shilingi bilioni 103 kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania imefikisha huduma zake Mkoani Mbeya na kuongeza kasi ya utoaji wa mikopo kutoka shilingi milioni 799.9 mwezi Desemba, 2017 hadi shilingi bilioni 2.54 kwa taarifa ya mwisho wa mwezi Aprili, 2019. Mikopo hiyo imetolewa kwa miradi saba ya kilimo na kuwanufaisha wakulima 509 wa Wilaya za Mbozi, Momba na Mbarali.

Napenda pia kulifahamisha Bunge lako tukufu kwamba Benki ya Maendeleo ya Kilimo imefanikiwa kufungua ofisi ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini Mkoani Mbeya. Malengo ya ufunguzi wa ofisi hiyo ni kuhakikisha kwamba benki inasogeza huduma zake karibu zaidi na wateja wake ambao ni wakulima wote wa Nyanda za Juu Kusini ikiwa ni pamoja na wakulima wadogo wa Wilaya ya Mbeya Vijijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutumia nafasi hii kuwahimiza wadau wote wa kilimo nchini ikiwa ni pamoja na wakulima wa Wilaya ya Mbeya Vijijini, kuwasiliana na Benki ya Maendeleo ya Kilimo ili waweze kupata maelekezo sahihi ya uandaaji wa miradi itakayokidhi vigezo vya kupatiwa mikopo na benki yao na pia kupatiwa maelezo ya fursa nyinginezo zinazopatikana katika benki yao.