Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 30 Energy and Minerals Wizara ya Nishat 252 2016-05-27

Name

Lameck Okambo Airo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rorya

Primary Question

MHE. DKT. RAPHAEL M. CHEGENI (K.n.y. MHE. LAMECK O. AIRO) aliuliza:-
Usambazaji wa umeme kupitia REA ulikusudiwa kufikishwa kwenye vijiji na senta 54 kwenye Awamu ya II na ingewezesha upatikanaji wa umeme asilimia 25-30, kwani upatikanaji wa umeme kabla ya mpango huo ulikuwa ni asilimia 5 na kwa kuzingatia mahitaji makubwa ya umeme kwa maendeleo ya wananchi wa Rorya umeme wa asilimia 25 bado ni wa chini na hata hivyo bado mradi unasuasua:-
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kuongeza kasi ya usambazaji umeme katika Wilaya ya Rorya?
(b) Je, ni lini Mpango wa REA II utakamilika na kuanza REA III?
(c) Je, REA III ina vijiji na senta ngapi ndani ya Wilaya ya Rorya?

Name

Dr. Medard Matogolo Kalemani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chato

Answer

NAIBU WAZIRI WA NISHATI NA MADINI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nishati na Madini, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Lameck Okambo Airo, Mbunge wa Rorya, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa REA Awamu ya II kwa Wilaya ya Rorya ulitarajia kufikisha huduma ya umeme katika vijiji 44. Mradi huu upo katika hatua mbalimbali za utekelezaji ambapo ujenzi wa njia kubwa ya umeme msongo wa kilovoti 33 na ufungaji wa transfoma umekamilika kwa asilimia 95 na wateja zaidi ya 300 katika vijiji 16 wameunganishiwa umeme kwa sasa. Ili kuhakikisha mradi unakamilika kwa muda uliopangwa, Serikali imeongeza kasi ya usimamizi wa karibu pamoja na kumwelekeza Mkandarasi Derm Electric kukamilisha kazi hizo kwa wakati.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa REA, Awamu ya II utakamilika mwishoni mwa Juni, 2016. Vijiji vitakavyobaki katika REA Awamu ya II vitaunganishiwa umeme kupitia REA Awamu ya III itakayoanza Julai, 2016.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, katika Wilaya ya Rorya, vijiji vipatavyo 56, sekondari nne na kanisa moja vinatarajiwa kupatiwa umeme katika Mpango wa REA Awamu ya III.