Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 5 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 63 2019-09-09

Name

Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AMINA S. MOLLEL aliuliza:-

ATM za Benki nyingi hapa nchini hazikidhi mahitaji ya watu wenye ulemavu:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kuhakikisha kuwa ATM za Benki zinawekewa mifumo inayokidhi mahitaji ya watu wenye ulemavu?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Amina Saleh Mollel, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, tangu Serikali ilipoanza maboresho ya mifumo ya malipo nchini mwaka 1996, Benki Kuu ya Tanzania imeendelea kusimamia usimikaji wa mifumo ya kisasa, mahiri na salama ili kuendana na mahitaji ya soko na mabadiliko ya teknolojia. Maboresho hayo ya mifumo yanalenga pamoja na mambo mengine kukidhi mahitaji ya makundi mbalimbali katika jamii wakiwemo watu wenye mahitaji maalum, hususan walemavu.

Mheshimiwa Spika, Mei, 2017 Benki Kuu ya Tanzania ilitoa mwongozo wa mfumo wa malipo kwa njia ya mtandao ikiwa ni mpango wa Serikali wa kuhakikisha kuwa huduma za malipo kwa njia ya mtandao yanafanyika kwa usalama na kukidhi mahitaji ya makundi yote katika jamii. Miongoni mwa vipengele muhimu na nyeti, hususan kwa watu wenye ulemavu vilivyoainishwa kwenye mwongozo huo ni alama za utambuzi, usalama wa mifumo na uwezo wa mifumo wa kutunza siri za wateja. Pamoja na Serikali kutoa mwongozo huo, benki zetu zote hapa nchini hazijafanikiwa kusimika ATM maalum na rafiki kwa watu wenye ulemavu, hususan watu wenye ulemavu wa macho. Hii ni kutokana na ukweli kwamba teknolojia ya ATM kwa watu wenye ulemavu wa macho ni ngeni na pia ina mfumo au mahitaji ya ziada ikilinganishwa na ATM za kawaida.

Mheshimiwa Spika, changamoto ya uduni wa baadhi ya miundombinu kwa watu wenye ulemavu, hususan walemavu wa miguu imetatuliwa kwa sehemu kubwa na hivyo kuwa rafiki katika maeneo mengi yanayotoa huduma za kibenki kwa kutumia mashine za ATM. Napenda kulihakikishia Bunge lako Tukufu kuwa Serikali itaendelea kufuatilia kwa karibu suala hili ili kuhakikisha kuwa mifumo ya miamala kwa njia ya ATM inakuwa rafiki kwa makundi yote wakiwemo watu wenye ulemavu.