Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 5 Finance and Planning Wizara ya Fedha na Mipango 61 2019-09-09

Name

Joyce Bitta Sokombi

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOYCE B. SOKOMBI aliuliza:-

Wafanyakazi wa Kiwanda cha MUTEX ambacho kilifungwa tangu mwaka 1984, wamekuja kulipwa stahiki zao Disemba, 2018 na badala ya kulipwa shilingi 400,000/= kwa gharama ya kila mwezi wakalipwa shilingi 100,000 tu:-

Je, Serikali haioni kuwa inawakandamiza wastaafu hao?

Name

Dr. Ashatu Kachwamba Kijaji

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kondoa

Answer

NAIBU WAZIRI WA FEDHA NA MIPANGO alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Joyce Bitta Sokombi, Mbunge Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali ilisimamisha uzalishaji katika kiwanda cha Nguo cha Musoma (Musoma Textile Mills Limited – MUTEX) mwaka 1994 baada ya kukabiliwa na changamoto ya ukosefu wa mtaji na ongezeko kubwa la madeni kutoka iliyokuwa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC). Kiwanda cha MUTEX kilifilisiwa na hatimaye kuuzwa mwezi Machi, 1998 kwa Kampuni ya LALAGO Cotton Ginnery and Oil Mills Company Limited.

Mheshimiwa Spika, kikao kati ya wadai, Serikali na Mfilisi kilifanyika Septemba 23, 2005 na kuridhia mapendekezo ya kulipa kiasi cha shilingi 161,347,359 kwa wafanyakazi 935 waliokuwepo kiwandani wakati Serikali ilipofanya uamuzi wa kusitisha uzalishaji. Maamuzi ya kulipa kiasi hicho cha fedha yalizingatia sheria, kanuni na taratibu za ufilisi.

Mheshimiwa Spika, baada ya zoezi la ufilisi kukamilika, wafanyakazi 512 pekee ndiyo waliojitokeza kuchukua mafao yao na wafanyakazi 423 waligoma kupokea mafao yao kwa madai kwamba, nauli ya familia na gharama za kusafirisha mizigo ni ndogo. Wafanyakazi hao 423 walifungua kesi katika Mahakama ya Kazi ya Tanzania, shauri la Uchunguzi wa Mgogoro Na. 49 wa mwaka 2007. Mahakama ilitoa tuzo mnamo tarehe 10 Juni, 2008 na kutupilia mbali shauri hilo na kuamuliwa wadai waende kwa Mfilisi kuchukua stahili zao.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, wafanyakazi hao hawakuridhika na uamuzi wa Mahakama na kufungua shauri lingine la kuomba marejeo katika Mahakama ya Kazi Tanzania shauri la Maombi ya Marejeo Na. 77 la Mwaka 2008. Mahakama hiyo ilitoa tuzo tarehe 15 Februari, 2010 na kutupilia mbali shauri la marejeo. Uamuzi ukabaki kuwa wafanyakazi hao 423 waliogoma kuchukua mafao yao waende kwa Mfilisi kuchukua stahili zao kama ilivyokubalika katika kikao cha wadau.

Mheshimiwa Spika, baada ya Serikali kupokea maombi ya malipo kutoka kwa wafanyakazi hao mwaka 2018, Ofisi ya Msajili wa Hazina ilifanya uhakiki wa wafanyakazi hao ili kujiridhisha na hatimaye kufanya malipo. Awali jumla ya wafanyakazi 219 walijitokeza na wasimamizi wa mirathi 14 na hivyo kulipwa jumla ya shilingi 44,591,559. Ofisi ya Msajili wa Hazina ilifanya tena zoezi la uhakiki mwezi Juni, 2019 kwa wafanyakazi ambao hawakujitokeza kwa uhakiki wa awali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Katika zoezi hilo, jumla ya wafanyakazi 115 walijitokeza tena pamoja na wasimamizi wa mirathi 27 ambao kwa ujumla wanastahili kulipwa shilingi 20,738,863. Ofisi ya Msajili wa Hazina inaendelea na taratibu za kulipa fedha hizo kwa wahusika katika mwaka huu wa Fedha 2019/2020. Aidha, Serikali inafuatilia kwa karibu malalamiko yote yanayohusu tofauti ya kiwango cha malipo yaliyofanyika hivi karibuni ikilinganishwa na kiwango kilichoidhinishwa kwenye kikao cha pamoja kati ya Mfilisi, wadau pamoja na Serikali kuona kama yana msingi na ukweli wowote.