Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 5 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 67 2019-11-11

Name

Devotha Methew Minja

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA M. MINJA aliuliza:-

Matukio ya watu kupoteza maisha kutokana na ajali za moto yamezidi kuongezeka nchini:-

Je, Serikali ina mpango gani wa kukiwezesha Kikosi cha Zimamoto ili kufanya kazi ipasavyo kwenye Miji na nje ya Miji?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Mathew Minja, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali inaendelea na jitihada za kuimarisha Jeshi la Zimamoto na Uokoaji ili liweze kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi. Pia, Serikali imekuwa ikitenga na itaendelea kutenga fedha za maendeleo katika bajeti ya Jeshi la Zimamoto na Uokoaji kila mwaka kwa ajili ya ununuzi wa magari ya kuzima moto pamoja na vifaa mbalimbali vya kuzima moto na uokoaji ili kutoa huduma zake ipasavyo ikiwemo kwenye miji na nje ya miji.

Mheshimiwa Spika, aidha, Serikali kupitia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji inashirikiana na Shirika la Nyumbu katika utengenezaji wa magari mapya ya kuzima moto na uokoaji. Pia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limesaini hati ya makubaliano na Kampuni ya ROM Solution ili kupata mkopo wenye masharti nafuu utakaowezesha kupata vitendea kazi mbalimbali ikiwemo magari ya kuzimia moto na uokoaji pamoja na vifaa nchi nzima.

Mheshimiwa Spika, pamoja na jitihada hizo nje ya Miji, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linaendelea kutoa elimu kwa Umma ya kuzuia na kupambana na majanga mbalimbali ili kuzuia na kupunguza matukio ya moto nchini. Pia, Serikali inaendelea kuwasisitiza wananchi kumiliki vizimia moto katika maeneo yao ili kuukabili moto katika hatua za awali.