Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 5 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 64 2019-11-11

Name

Mbarouk Salim Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Wete

Primary Question

MHE. MBAROUK SALIM ALI aliuliza:-

Pemba ni Kisiwa kinachozalisha viungo (spices) kwa wingi na wajasiriamali huzalisha bidhaa zinazotokana na viungo hivyo:-

Je, ni lini wakulima na wajasiriliamali wa Pemba wataunganishwa na soko la Afrika Mashariki ili waweze kufaidika na soko hilo?

Name

Dr. Advocate Damas Daniel Ndumbaro

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, napenda kujibu swali la Mhe. Mbarouk Salim Ali, Mbunge wa Wete kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, napenda kumtaarifu Mhe. Mbunge kuwa, wananchi wa Pemba na wa maeneo yote ya Tanzania wamekwisha unganishwa na soko la Afrika Mashariki kupitia Itifaki za Umoja wa Forodha na ya Soko la Pamoja la Afrika Mashariki.

Mheshimiwa Spika, kwa mkulima au mjasiriamali yoyote kuweza kuuza bidhaa zake ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki anapaswa kukidhi vigezo vya Afrika Mashariki vya kutambua uasili wa bidhaa (Rules of Origin). Nchi Wanachama zilikubaliana na kuweka vigezo vinavyoshabihiana kama bidhaa husika imezalishwa ndani ya Jumuiya ya Afrika Mashariki. Vigezo hivyo vimejengwa katika misingi ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, bidhaa kuzalishwa ndani ya Jumuiya kwa kiwango cha asilimia mia moja mfano, bidhaa za kilimo, uvuvi, madini na kaadhalika; bidhaa kuzalishwa ndani ya Jumuiya kwa kutumia malighafi ya kutoka nje yenye thamani (ex-works price) ya kiwango kisichozidi asilimia 70 ya bei ya bidhaa hiyo bila kodi ikiwa kiwandani, mfano label za plastik, kuongeza ugumu wa kioo, utengenezaji wa nyaya za umeme na vifaa vingine vya umeme, utengenezaji wa pikipiki na baskeli n.k; bidhaa zinazozalishwa ndani kwa kutambua mchakato katika uzalishaji (process rule) kama vile uunganishaji wa magari na kusafisha mafuta ya petroli (refining); na bidhaa kubadilika utambuzi wa uasili kwa kubadilika umbo na matumizi kutokana na mchakato wa viwandani mfano malighafi ya plastiki kuchakatwa kuwa meza, viti, sahani n.k.

Mheshimiwa Spika, kwa kuzingatia misingi ambayo nimekwisha ielezea hapo juu, nichukue fursa hii kupitia Bunge lako Tukufu kuwashauri wananchi wa Pemba na Tanzania kwa ujumla kuzichangamkia fursa za kibiashara, ajira, uwekezaji n.k. zitokanazo na Jumuiya ya Afrika Mashariki katika kujihakikishia maendeleo.

Mheshimiwa Spika, vilevile, kuwasihi wananchi kuzitambua taratibu za kufuata katika kuzitumia fursa za kibiashara zilizopo katika Jumuiya ya Afrika Mashariki ikiwa ni pamoja na kuwa na cheti cha Uasili wa Bidhaa (East African Communicate Certificate of Origin) na vibali/ nyaraka zinazobainisha kuwa bidhaa imezalishwa ndani ya Jumuiya kutoka mamlaka husika kutegemea na aina ya bidhaa mfanyabiashara anazotaka kuuza/kununua katika soko la Afrika Mashariki.