Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 4 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 44 2019-11-08

Name

Pauline Philipo Gekul

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Primary Question

MHE. PAULINE P. GEKUL aliuliza:-

Miundombinu mibovu ya barabara zinazoelekea Hifadhini husababisha Watalii kuwa wachache Mathalan; barabara inayotoka Iringa Mjini hadi Hifadhi ya Ruaha kilometa 104 ni ya vumbi na vilevile barabara ya kutoka Babati Mjini hadi Tarangire kilometa 20 ni ya vumbi:-

Je, ni lini Serikali itajenga barabara hizo kwa kiwango cha lami ili kuwavutia Watalii wengi zaidi?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii naomba kujibu swali la Mheshimiwa Pauline Philipo Gekul, Mbunge wa Babati Mjini kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya kutoka Iringa Mjini kuelekea Hifadhi ya Taifa Ruaha ambayo inajulikana kama barabara ya Iringa – Msembe ni barabara ya Mkoa inayosimamiwa na Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano kupitia Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADs) Mkoa wa Iringa. Barabara hii ina urefu wa kilomita 104 kati ya hizo kilomita 18.4 ni za lami na kilomita 85.6 ni za changarawe. Barabara hii inapitia katika maeneo muhimu ya makumbusho ya Mtwa - Mkwawa (Kalenga), maeneo yenye kilimo cha Mpunga na Mahindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kutambua umuhimu wa barabara hii, TANROADs imefanya Upembuzi yakinifu, Usanifu wa kina na kuandaa makabrasha ya zabuni kwa ajili ya ujenzi kwa kiwango cha lami. Kazi hii imefanywa na Mhandisi Mshauri M/s ENV Consult (T) Ltd wa Dar es Salaam na tayari imekamilika. Ambapo jumla ya shilingi billioni 4.22 zimetengwa Katika mwaka wa fedha 2019/2020 kwa ajili ya maandalizi ya kuanza ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu kupitia Taasisi zake imekuwa ikishirikiana na Mamlaka zingine kuhakikisha kwamba barabara mbalimbali zinazoelekea maeneo ya Hifadhi zinapitika wakati wote kwa kufanya ukarabati wa mara kwa mara. Kwa mfano, Hifadhi ya Taifa Tarangire imeshirikiana na TARURA kurekebisha barabara ya kutoka Minjingu kwenda Tarangire yenye urefu wa kilometa 7 na barabara ya kutoka lango la Sangaiwe kwenda kijiji cha Usole – Mwada – Sangaiwe kwa kufanya matengenezo ya kuchonga na kuweka moram.

Mheshimiwa Mwenyekiti, aidha, usanifu wa barabara ya Minjingu – Tarangire kilometa saba kwa kiwango cha lami umekamilika na sasa inatafutwa fedha kwa ajili ya ujenzi. Barabara kutoka Babati Mjini hadi Hifadhi ya Taifa Tarangire kilomita 20 inafanyiwa ukarabati wa mara kwa mara kila mwaka kwa ushirikiano kati ya TARURA na Hifadhi ya Taifa Tarangire.