Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 4 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 41 2019-11-08

Name

Vedastus Mathayo Manyinyi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Musoma Mjini

Primary Question

MHE. VEDASTUS M. MANYINYI aliuliza:-

Ikiwa lengo la Serikali ni kuhakikisha inawahudumia na kutatua kero za wananchi, kero hizo zisipotatuliwa katika ngazi za Mitaa, Kata, Wilaya na Mkoa wananchi hao hulazimika kuandika na kushika mabango kila Mheshimiwa Rais anapofika majimboni ili kupaza sauti zao:-

(a) Je, ni kwa nini Viongozi wa Wilaya na Mkoa huzuia mabango hayo yasionekane na kusomwa na Mheshimiwa Rais?

(b) Je, wananchi watumie njia gani kufikisha ujumbe wao kwa Mheshimiwa Rais pale matatizo yanaposhindwa kutatuliwa katika ngazi ya chini?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MIAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Vedastus Mathayo Manyinyi, Mbunge wa Musoma Mjini lenye sehemu (a) na (b), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Serikali kwa ujumla inaamini katika uwazi na uwajibikaji na kwamba, ni haki ya msingi ya wananchi kueleza matatizo yao kwa sauti au kwa maandishi pindi wanapotembelewa na Viongozi mbalimbali wa Kitaifa ikiwa ni pamoja na Mheshimiwa Rais. Kama kuna Viongozi wa Mikoa au Wilaya wanawazuia wananchi, hayo sio maelekezo ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI wala Serikali na wanapaswa kuacha mara moja tabia hiyo kwa kuwa, wananchi wana haki ya kueleza changamoto zao kwa Viongozi wa Kitaifa.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inao utaratibu na mfumo wa kuhakikisha kero za wananchi zinatatuliwa na viongozi. Mfumo huo unaanzia ngazi ya Kitongoji hadi Taifa, utaratibu ambao unawawezesha wananchi kufikisha kero zao kwenye ngazi mbalimbali kwa ajili ya kuzitafutia utatuzi. Nazielekeza Halmashauri na Sekretarieti za Mikoa kuimarisha madawati ya kupokea kero na malalamiko katika maeneo yao ili kuwawezesha wananchi kufikisha kero na changamoto zao kwa wakati. Ahsante.