Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 3 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 30 2019-11-07

Name

Ezekiel Magolyo Maige

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Msalala

Primary Question

MHE. NAPE M. NNAUYE (K.n.y. MHE. EZEKIEL M. MAIGE) aliuliza:-

Wananchi wa Msalala kwa juhudi zao wamejenga mabweni katika Shule za Sekondari za Bulige, Busangi, Baloha, Mwalimu Nyerere, Lunguya, Ntobo na Isaka.


(a) Je, Serikali ipo tayari kuunga mkono juhudi hizo za wananchi kwa kuyatambua mabweni hayo na kuzipatia shule hizo ruzuku za uendeshaji wa mabweni kwa ajili ya umeme, maji, chakula na ulinzi?

(b) Je, Serikali ipo tayari kuongeza miundombinu kama mabwalo ya chakula na nyumba za matron katika Shule hizo?

(c) Je, ni lini Serikali itasaidia wasichana wa Msalala katika Kata nyingine kama Mwanase, Mwalugulu, Jana, Bugerema na Bulyanhulu kwa kuwajengea Mabweni?

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. MWITA M. WAITARA) alijibu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ezekiel Magolyo Maige, Mbunge wa Msalala, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa Serikali kugharamia shule za bweni na shule za kutwa ni tofauti. Shule zilizotajwa na Mheshimiwa Mbunge ni za kutwa ambazo hupelekewa fedha za fidia ya ada na fedha uendeshaji. Ili shule hizo ziweze kupelekewa fedha kwa ajili ya chakula, ni lazima ziwe zimesajiliwa kama shule za bweni za Kitaifa. Shule za Kitaifa zina sifa ya kuchukua wanafunzi kutoka Mikoa yote ya Tanzania Bara na hushindanishwa kutokana na ufaulu wao.

(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuongeza miundombinu ya mabweni na mabwalo ya chakula kwenye shule hizo, kwa sasa kipaumbele cha Serikali ni kuongeza mabweni na mabwalo kwenye shule za bweni na kuongeza madarasa, maabara na matundu ya vyoo kwenye shule za kutwa. Katika mwaka fedha 2018/2019, Halmashauri ya Wilaya ya Msalala imepatiwa kiasi cha shilingi milioni 100 kwa ajili ya ukamilishaji wa maboma ya madarasa nane katika shule nne za sekondari. Vilevile, katika mwaka wa fedha 2019/ 2020 kupitia program ya EP4R, Serikali imetenga kiasi cha shilingi bilioni 58.2 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya shule za sekondari nchini.

(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, Mpango wa Serikali ni kuboresha miundombinu katika shule zote za Serikali. Nazielekeza Halmashauri ziendelee kushirikiana na wananchi na wadau mbalimbali wa maendeleo kujenga hosteli kwenye shule zilizoko katika maeneo yao ili kuboresha mazingira ya kujifunzia na kujifunzia kwa watoto wa kike nchini. Ahsante.