Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 2 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 20 2019-11-06

Name

Angelina Adam Malembeka

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza:-

Majanga ya moto yamekuwa yakitokea mara kwa mara hasa Viwandani, Majumbani na katika majengo ya Serikali:-

(a) Je, Serikali ina mkakati gani wa kutoa mafunzo kwa Wafanyakazi na wananchi juu ya mbinu za kujihami na kujiokoa katika majanga ya moto?

(b) Je, Serikali imejipangaje katika kutoa mafunzo katika maeneo ya kazi na wananchi juu ya matumizi ya mitungi ya kuzima moto (Fire Extinguishers)?

(c) Je, Serikali ina mpango gani wa kukagua mitungi hiyo kama bado inafaa kwa matumizi au imeshapita muda wake wa kutumika?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Kaskazini Unguja, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji linaendelea kutoa mafunzo ya mbinu za kujihami na jinsi ya kujiokoa katika majanga ya moto kwenye maeneo ya kazi na wananchi kwa ujumla. Elimu dhidi ya kinga na tahadhari ya moto imeendelea kutolewa katika maeneo mbalimbali nchini ikiwemo maeneo yenye mikusanyiko ya watu kama vile masoko, Shule za Sekondari na Msingi, Vyuo, Makanisani na Misikitini kupitia vyombo mbalimbali vya habari vikiwemo magazeti, radio na televisheni.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Jeshi la Zimamoto na Uokoaji limejipanga vyema kutoa mafunzo kwenye maeneo ya kazi na wananchi juu ya matumizi ya mitungi ya kuzimia moto kwa kuanzisha kampeni mbalimbali kama vile “Ninacho, Ninajua Kukitumia,” “Mlango kwa Mlango” na “Nyumba Salama” zenye lengo la kuhamasisha watu kuwa na vizimia moto na kujua kuvitumia katika maeneo ya makazi, viwanda, maeneo ya vyombo vya usafiri na usafirishaji, majumbani, maeneo ya biashara na katika mikusanyiko mikubwa ya watu. Aidha, wananchi wanaendelea kupatiwa elimu na mafunzo juu ya mifumo yote ya kuzima kuzima katika majengo na maeneo mbalimbali ili kuepusha majanga ya moto.

(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Ukaguzi wa tahadhari na kinga dhidi ya moto kwa mujibu wa Kanuni za Jeshi la Zimamoto na Uokoaji umeendelea kufanyika sambasamba na ukaguzi wa mitungi ya kuzima moto na kumshauri mtumiaji juu ya ubora wa mtungi na kumshauri mmiliki ipasavyo.