Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 1 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 12 2019-11-05

Name

Kiteto Zawadi Koshuma

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. STANSLAUS S. MABULA (K.n.y. MHE. KITETO Z. KOSHUMA) aliuliza:-

Bodi ya Utalii pamoja na mambo mengine ina jukumu la kutunza utalii wa ndani ya nchi:-

Je, Serikali inasimamiaje Bodi hiyo ili kuhakikisha Mkoa wa Mwanza unatangazwa kama Mji wa Kitalii?

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimisha Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiteto Zawadi Koshuma, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, katika kuhakikisha kuwa vivutio vya utalii vilivyopo Mkoani Mwanza vinatangazwa ipasavyo, Wizara inayo ofisi ya kanda ya Idara ya Utalii Jijini Mwanza na mwaka 2011 ilielekeza Bodi ya Utalii Tanzania (TTB) kufungua Ofisi ya Kanda jijini Mwanza. Aidha, Wizara imeelekeza Shirika la Hifadhi za Taifa Tanzania - TANAPA kufungua Ofisi ya kanda ya kaskazini magharibi Mkoani Mwanza. Lengo likiwa si tu kusogeza karibu huduma kwa wadau wa sekta ya utalii lakini pia kuhakikisha vivutio vya utalii na fursa za uwekezaji katika sekta ya utalii Mkoani Mwanza na maeneo yote ya kanda ya Ziwa zinatangazwa kikamilifu.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo Wizara yangu kwa kushirikiana na Sekta binafsi imekuwa ikishiriki na kuratibu matukio na matamasha yanayolenga kutangaza vivutio vya Mkoani Mwanza ikiwemo; Maadhimisho ya Siku ya Utalii Duniani, Tamasha la Bulabo na Afro Calabash, Tamasha la Urithi (Urithi Festival), Rocky City Marathon na Mashindano ya Urembo. Lengo ni kuvutia wageni na watalii wa ndani na nje kutembelea mikoa hiyo.

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu inatambua kuwa Mkoa wa Mwanza ni miongoni mwa maeneo machache yenye rasilimali nyingi za utalii ikiwemo fukwe nzuri za Ziwa Viktoria, visiwa vinavyovutia, Hifadhi ya Taifa ya Saanane, wanyamapori, utamaduni, miamba ya mawe yenye kuvutia na mandhari nzuri ya jiji. Vivutio hivi kwa miaka ya karibuni vimekuwa vivutio wageni wengi kutembelea mkoa huo.

Mheshimiwa Spika, Kwa sasa Wizara inaendesha zoezi la kubainisha vivutio vya utalii kwa dhumuni la kuviendeleza na kuvitangaza. Katika mwaka wa Fedha 2019/2020 Wizara imelenga kutekeleza zoezi hilo katika Mikoa sita ikiwemo Mkoa wa Mwanza. Kazi hii inatekelezwa kwa kushirikiana na Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), uongozi wa mkoa, Wilaya, Vijiji na wadau wa sekta ya utalii.

Mheshimiwa Spika, aidha, tarehe 16 na 17 Machi, 2019 Wizara ilifanya kikao na wadau wa utalii kanda ya ziwa na magharibi ikiwa ni jitihada za kuimarisha utalii Mkoani Mwanza na Kanda ya ziwa kwa ujumla. Katika kikao hicho kilichofanyika Mkoani Mwanza kilihusisha viongozi kutoka Mikoa ya Mwanza, Geita, Simiyu, Mara, Kagera, Shinyanga na Kigoma. Vilevile Wizara inaendelea na jitihada zingine za kuhamasisha uwekezaji kwenye shughuli za utalii na vijana kujifunza uongozaji watalii katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, Sekta ya utalii ni mtambuka, hivyo kazi ya utangazaji na uendelezaji sekta hii inahitaji juhudi za pamoja za wadau wa sekta ya umma na binafsi. Nitoe wito kwa Mheshimiwa Mbunge na Uongozi wa Mkoa wa Mwanza kuendelea kufanya kazi kwa karibu na Wizara yangu katika jitihada za kuendeleza na kutangaza vivutio vya utalii vya Mkoa wa Mwanza.