Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 1 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 11 2019-11-05

Name

Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Primary Question

MHE. AUGUSTINO M. MASELE aliuliza:-

Mikoa ya Kanda ya Ziwa imeathirika na mabadiliko ya tabia nchi na uharibifu mkubwa wa mazingira:-

Je, ni lini Serikali itajenga vyuo vya uhifadhi wa wanyamapori na uhifadhi wa mazingira na elimu ya utalii hasa baada ya kuanzishwa kwa hifadhi za Taifa Burigi- Chato, Kigosi, Ibanda – Rumanyika, Rubondo na Hifadhi ya Taifa ya Mto Ugalla.

Name

Constantine John Kanyasu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Geita Mjini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Agustino Manyanda Masele, Mbunge wa Mbogwe kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara yangu ina vyuo vinavyotoa mafunzo katika fani za uhifadhi wa wanyamapori, utalii na misitu ambapo uhifadhi wa mazingira ni sehemu ya mafunzo hayo. Mafunzo hutolewa katika ngazi za astashahada, stashahada, shahada na elimu nyingine za juu.

Mheshimiwa Spika, kwa mfano, Chuo cha Pasiansi kilichopo Kanda ya Ziwa katika Mkoa wa Mwanza kinatoa Astashahada ya awali ya uhifadhi wa wanyamapori na himasheria, na Stashahada ya uhifadhi wa wanyamapori na himasheria, Chuo cha Wanyamapori - MWEKA kilichopo Kilimanjaro, kinatoa Astashahada na Shahada ya uhifadhi wa wanyamapori na utalii. Chuo cha mafunzo ya Uhifadhi wa maliasili kwa jamii - Likuyu Sekamaganga kilichopo Mkoa wa Ruvuma, Wilaya ya Namtumbo kinatoa mafunzo kuhusu mbinu za kudhibiti wanyamapori wakali na waharibifu kwa askari wanyamapori wa vijiji (VGS), viongozi na wajumbe wa Kamati za Maliasili za vijiji.

Mheshimiwa Spika, Wizara kupitia Chuo cha Misitu Olmotonyi kinatoa mafunzo yanayohusu misitu katika ngazi za astashahada na stashahada pamoja na mafunzo ya ufugaji nyuki katika chuo cha Ufugaji Nyuki – Tabora. Vilevile, Wizara kupitia Chuo cha Viwanda vya Misitu kilichopo Moshi hutoa mafunzo ya teknolojia ya viwanda vya misitu katika ngazi ya astashahada ya awali, astashahada na stashahada.

Mheshimiwa Spika, pia Wizara kupitia Chuo cha Taifa cha Utalii inatoa mafunzo ya utalii, ukarimu na uongozaji watalii katika ngazi za Astashahada na Stashahada.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa Serikali inaendelea kuimarisha vyuo vilivyopo na haina mpango wa kujenga chuo kipya ili kukidhi mahitaji ya nchi nzima.