Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 17 Sitting 1 Energy and Minerals Wizara ya Madini 5 2019-11-05

Name

Agnes Mathew Marwa

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. AGNESS M. MARWA aliuliza:-

Wananchi wengi walibomolewa nyumba zao na Mgodi wa ACACIA uliopo Nyamongo, Wilayani Tarime na wengine hawajalipwa fidia ya maeneo yao mpaka sasa. Aidha, mgodi pia umeanza kuchimba chini ya maeneo ya watu (Underground mining):-

Je, ni lini mgodi wa ACACIA uliopo Nyamongo utalipa fidia kwa wananchi hawa?

Name

Doto Mashaka Biteko

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bukombe

Answer

WAZIRI WA MADINI alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Agness Mathew Marwa, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kusimamia sekta ya madini kwa kuhakikisha uwekezaji unafanyika kwa mujibu wa sheria na taratibu za nchi ikiwemo kuhakikisha kuwa wananchi wanaoishi katika maeneo ambayo miradi ya uendelezaji migodi inataka kufanyika na kulazimika kupisha maeneo yao wanalipwa fidia stahiki kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi na wanapewa makazi mbadala ambayo yana hali bora zaidi kuliko makazi waliyokuwa nayo awali.

Mheshimiwa Spika, uthaminishaji katika maeneo yanayozunguka mgodi wa North Mara na ulipaji wa fidia umegawanyika katika awamu nyingi kwa kuzingatia vijiji husika kuridhia. Kijiji cha Nyabirama chenye wakazi 1,974 waliothaminiwa katika awamu ya 20, 35 na 42 wote walilipwa fedha zao isipokuwa wakazi 64 ambao fedha yao iliyoidhinishwa ya shilingi bilioni 1.9 waliikataa hundi zao zikabaki Ofisi ya Mkurugenzi Wilaya ya Tarime. Eneo la Nyabichune lilithaminiwa katika awamu ya 47 kwa kuidhinisha shilingi milioni 224 kwa ajili ya watu 69. Wizara iliagiza uthamini wa maeneo hayo ya Kijiji hicho cha Nyabichune urudiwe kwa sababu wananchi wale walionekana wamepunjwa. Mthamini Mkuu wa Serikali ameshakamilisha uthaminishaji wa maeneo 1,838 ambayo tayari umeshawasilishwa kwenye menejimenti ya mgodi kwa hatua zake za ulipaji.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la mgodi kubadilisha aina ya uchimbaji toka uchimbaji wa wazi (open pit) kwenda underground mining, uamuzi huo ulifikiwa baada ya mgodi huo kufanya utafiti ulioonesha kuwa gharama ya uchimbaji wa chini zilikuwa ndogo ukilinganisha na uchimbaji wa mgodi wa wazi. Naomba niwatoe shaka wana Tarime kuwa Wizara inafuatilia kwa karibu uchimbaji unaofanyika na mpaka sasa uchimbaji wa underground unafanyika katika eneo la Gokona kuelekea Nyabigena ndani ya maeneo waliyokuwa wakichimba toka awali. Hivyo, hakuna eneo ambalo mgodi wa underground unachimba kwenye makazi ya watu.