Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 8 Regional Administration and Local Government Authorities Ofisi ya Rais TAMISEMI. 96 2020-02-06

Name

Julius Kalanga Laizer

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Monduli

Primary Question

MHE. JULIUS K. LAIZER aliuliza:-

Mji wa Mto wa Mbu ni mji wa kitalii na unaingiza mapato mengi ya kitalii; lakini unakabiliwa na tatizo la miundombinu ya barabara;

(a) Je nini mkakati wa Serikali kuupatia Mji wa Mto wa Mbu angalau km 5 za lami?

(b) Je Serikali ina mpango gani wa kuanza ujenzi wa barabara ya Mto wa Mbu mpaka Loliondo kwa kiwango cha lami ili kusaidia mradi wa kimkakati wa magadi Engaruka?

(c) Je ni lini Serikali itatimiza ahadi ya Mhe. Rais ya kuweka lami barabara ya Ngarasha mpaka Monduli Juu kwa Sokoine?

Name

Josephat Sinkamba Kandege

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kalambo

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA (MHE. JOSEPHAT S. KANDEGE) alijibu:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Julius Kalanga Laizer, Mbunge wa Monduli, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-

(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali kupitia Wakala wa Barabara za Vijijini na Mijini – TARURA imekamilisha usanifu wa barabara za Mji Mdogo wa Mto wa Mbu kwa kiwango cha lami zenye jumla ya urefu wa kilometa 9 ambazo ujenzi wake utagharimu jumla ya shilingi bilioni 7.32. Serikali inatafuta fedha kwa ajili ya ujenzi ambao utafanyika kwa awamu.

(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Mto wa Mbu – Loliondo ina urefu wa kilometa 247 na ipo chini ya Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS). Serikali imeanza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami. Katika mwaka wa fedha 2019/20 kiasi cha Shilingi bilioni 87 kimetolewa kwa ajili ya kujenga kipande chenye urefu wa kilometa 49 na ujenzi umefikia asilimia 43. Serikali itaendelea kujenga barabara hii kwa awamu kwa kadri ya upatikanaji wa fedha.

(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Barabara ya Ngarasha mpaka Monduli Juu kwa Sokoine yenye urefu wa kilometa 11.66 iko chini ya Wakala wa Barabara Tanzania (TANROADS). Wakala wa Barabara unaendelea na usanifu wa barabara hiyo. Kwa sasa Serikali inaendelea kutafuta fedha kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo unaotarajia kuanza pindi usanifu wa barabara hiyo utakapo kamilika.